September 30, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mkurugenzi wa TAMWA, Rose Reuben

TAMWA yazindua mafunzo ya Mradi wa Wanawake Wanaweza

Na Angela Mazula, TimesMajira Online, Dar es Salaam

CHAMA cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) kupitia Mradi wa Wanawake Wanaweza, kimezindua mafunzo kwa waandishi wahabari 50 wa redio za kijamii kutoka mikoa 17 ya Tanzania Bara.

Mradi huo unaofadhiliwa na Shirika la Umoja wa Mataifa linalohudumia Wanawake (Un Women) unalenga kuwajengea uwezo wa namna ya kuripoti kuhusu ushiriki wa wanawake katika suala zima la uongozi ili kuondoa mifumo kandamizi inayochochea ukatili wa wanawake na kuwakosesha fursa mbalimbali za uongozi katika nyanja za kiuchumi,kijamii na kisiasa.

Akizungumza na waandishi wa habari wakati wa uzinduzi wa mradi huo, Mkurugenzi Mtendaji wa TAMWA, Rose Reuben alisema jamii imezungukwa na mila na desturi kandamizi ambazo zimesababisha wanawake kuwa kundi B katika ngazi za uongozi.

“Wanawake hawaaminiwi na jamii kuwa wanaweza kuwa viongozi sasa mifumo hii mbaya zaidi imewafanya wao wenyewe kutojiamini kabisa na kuona kama ni wanaume pekee ndiyo wana haki ya kuwania nafasi za uongozi, jambo ambalo halina ukweli,” alisema Reuben.

Aidha ameongeza kuwa baada ya mafunzo hayo waandishi wa habari za redio hizo wataenda kuandaa vipindi vya redio vitakavyoelimisha na kutambulisha wanawake kuwa wanastahili kuwa viongozi halali.

“Mbali na hilo, TAMWA itawakutanisha wanahabari na wahabari nguri kwa ajili ya ushauri wa namna ya kuandika habari zitakazoleta matokeo katika mradi kwa kufuata maadili ya uandishi wa habari, na kutumia midahalo ya kihabari kuongeza uelewa kwa jamii na ushiriki wa wanawake katika uongozi na siasa,” amesema Reuben na kuongeza;

Hata hivyo kwa kutumia redio za kijamii maana huko kuna wasikilizaji wengi na ujumbe utafika kwa urahisi pembezoni mwa Tanzania ambapo huenda hawapati elimu hiyo kwa wakati.”

Katika maeneo yatakayotumika kama sampuli ya utekelezaji wa mradi huo ni mikoa 17 ambayo ni Dar es salaam, Pwani, Morogoro, Dodoma, Singida, Tabora, Shinyanga na Mwanza.

Mingine ni Mara, Mbeya, Ruvuma, Lindi na Mtwara na Wilaya zake 112 za mikoa hiyo na kata 458.