June 17, 2026

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Ridhiwani aipongeza mchango wa TEA kwenye Elimu

Na Joyce Kasiki, Dodoma

WAZIRI  wa Nchi, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Ridhiwani Kikwete, ameipongeza Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) kwa huduma mbalimbali inazotoa kwa wananchi na kuitaka kuongeza kasi ya kuelimisha umma kuhusu juhudi zinazofanywa na Serikali katika kuboresha sekta ya elimu nchini.

Ridhiwani alitoa pongezi hizo alipotembelea banda la Mamlaka ya Elimu Tanzania katika Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali Park jijini Dodoma, ambapo alipata fursa ya kujionea huduma na shughuli mbalimbali zinazotekelezwa na taasisi hiyo.

Akizungumza alipotembelea banda hilo la  TEA, Ridhiwani alisema taasisi hiyo ina mchango mkubwa katika maendeleo ya elimu nchini kupitia usimamizi wa Mfuko wa Elimu wa Taifa, hivyo ni muhimu wananchi wakaendelea kupata taarifa sahihi kuhusu miradi na mafanikio yanayotekelezwa kwa manufaa yao.

Kwa upande wake, Afisa Uhusiano na Mawasiliano wa Mamlaka ya Elimu Tanzania, Eliafile Solla, alisema ushiriki wa TEA katika maadhimisho hayo unalenga kutoa elimu kwa wananchi kuhusu majukumu na shughuli mbalimbali zinazotekelezwa na mamlaka hiyo kupitia Mfuko wa Elimu wa Taifa.

Ametaja  majukumu makuu mawili yya TEA ambayo ni kutafuta rasilimali fedha na vifaa kutoka kwa wadau mbalimbali wa maendeleo na kisha kugawa rasilimali hizo katika shule na taasisi za elimu kwa lengo la kuboresha miundombinu ya kufundishia na kujifunzia nchini.

“Tunatumia maonesho haya kuwafikia wananchi moja kwa moja ili waelewe namna TEA inavyoshirikiana na wadau mbalimbali katika kuimarisha sekta ya elimu kwa kutoa rasilimali zinazosaidia ujenzi na ukarabati wa miundombinu ya elimu pamoja na upatikanaji wa vifaa vya kujifunzia na kufundishia,” amesema Solla.

Ameongeza kuwa watumishi wa TEA walioshiriki maonesho hayo wamejipanga kutoa elimu kwa wananchi wanaotembelea banda hilo, sambamba na kuendelea kutekeleza jukumu la kutafuta rasilimali fedha na vifaa vitakavyosaidia kuimarisha juhudi za Serikali za kuboresha mazingira ya elimu nchini.