Na Mwandishi Wetu,Timesmajira Online
MAHAKAMA Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi, imewahukumu kifungo cha maisha jela Suleiman Thabit Ngulangwa na Farid Hamis Said.
Hukumu hiyo imekuja baada ya washtakiwa hao kutiwa hatiani kwa kosa la biashara haramu ya dawa za kulevya aina ya heroin yenye uzito wa kilo 15.19.
Katika hukumu iliyotolewa Juni 1, 2026, Jaji S.E. Kisanya amesema ushahidi wa upande wa mashtaka ulithibitisha pasipo shaka kuwa washtakiwa hao walikuwa na umiliki wa dawa hizo.

Mchambuzi wa Serikali kutoka Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali (GCLA), Leonidl Michael ameithibitishia mahakama kuwa pakiti 16 zilizokamatwa zilikuwa na heroin yenye uzito wa kilo 15.19 baada ya kufanyiwa uchunguzi wa kisayansi.
Mahakama ilibaini kuwa utetezi wa washtakiwa haukuweza kuibua shaka dhidi ya ushahidi wa mashahidi na vielelezo vilivyowasilishwa.
Mshtakiwa wa pili, Sharifa Selemani Bakari, aliachiliwa huru baada ya mahakama kubaini kuwa upande wa mashtaka haukuthibitisha ushiriki wake katika kosa hilo.

Mbali na kifungo hicho, mahakama imeagiza heroin yote iliyokamatwa pamoja na vifaa vya kufungashia kuteketezwa kwa mujibu wa sheria.

More Stories
Jukwaa la Biashara la Viwango kufanyika Juni 5
CCM waibuka kidedea Udiwani kata ya Kala
Mtatifikolo (CCM) aibuka kidedea jimbo la Isimani