April 23, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

86 wahitimu mafunzo ya BRAC

Mwandishi Wetu, TimesMajira Online

KATIKA kuhakikisha mtoto wa kike anakombolewa ili aweze kufikia malengo yake Shirika linapojishughulisha na masuala mbalimbali ikiwemo kutoa mikopo kwa wanawake na elimu BRAC Maendeleo Tanzania limetoa vyeti kwa wanafunzi 86 ambao wamehitimu Mafunzo ya kozi fupi mbalimbali za ufundi stadi.

Mafunzo hayo yanayotolewa bure, yaliwalenga zaidi watoto wa kike ambao walipata fursa ya kujifunza mambo mbalimbali ikiwemo Mapishi, urembo, Upambaji na ushonaji vitakavyowawezesha kujiajiri.

Akizungumza katika mahafali ya kuwatunukia vyeti wanafunzi hao, Mkurungezi wa BRAC International Afrika, Lucy Okowa amewataka wahitimu hao kutumia vyema Mafunzo waliyoyapata ili waweze kutimiza ndoto zao za badae.

Okowa amesema, wanafunzi hao wamenuafaika na Mafunzo hayo chini ya mradi wa ELA ambao umelenga kumnyanyua mtoto wa kike na kumuwezesha kumudu maisha yake kiuchumi na kijamii na kufanikiwa na badae kumaliza mafunzo na kupata msaada wa vifaa mbalimbali

Mkurugenzi wa upande wa Africa kutoka BRAC International, Ruth Okowa akisikiliza maelezo kutoka kwa mmoja wa mabinti wanaonufaika na mradi wa ELA unaotekelezwa na BRAC Maendeleo Tanzania. Kulia kwake ni Mkurugenzi wa BRAC Maendeleo Tanzania, Susan Bipa.

Amesema, wanawake duniani kote wamekuwa wakisifika kwa kuwa watu wenye ustahimilivu na kujitolea kwa nguvu zao zote katika kuhakikisha familia zao zinasonga mbele.

“BRAC Maendeleo Tanzania ina amini kuwa ilikuleta mabadiliko chanya katika jamii na kuinua familia kwa ujumla ni muhimu kumuwezesha mwanamke kwa sababu daima mwanamke hashindwi na jambo,”amesema.

Pia amewataka wahitimu hao wanapoanza safari ya ujasiriamali wawe makini ikiwa ni pamoja na kuzingatia mafunzo mbalimbali waliyoyapata katika kipindi chote cha mafunzo.

“Ujasiriamali sio lelemama nawaomba muwe wavumilivu chagamoto nyingi mtapitia lakini msikate tamaa kila unapofeli nyanyuka, jifunze kutokana na makosa na uendelee kukaza mwendo kwa sababu wanawake sio jadi yetu Kushindwa,” amesisitiza Okowa.

Baadhi ya washiriki wa mradi wa ELA unaotekelezwa na shirika la BRAC Maendeleo Tanzania wakionyesha nguo walizoshona baada ya kumalizika kwa mafunzo yao waliyokuwa wakipata kutoka Chuo cha Ufundi Temeke wakati wa hafla iliyofanyika katika chuo hicho na kupatiwa vifaa vya ujasiriamali ili kujikwamua kiuchumi.

Elina Patrick ambaye ni mmoja wa wanafunzi walionufaika na mafunzo hayo katika eneo la Upambaji amesema, mafunzo aliyoyapata yatamsaidia kujikwamua na kujiajiri mwenyewe na kumuwezesha kupata kipato cha kumudu maisha yake.

“Matarajio yangu ni kufungua saluni yangu mwenyewe ambayo itanisaidia kutegeneza kipato ambacho kitanisaidia mimi na familia yangu lakini pia ndoto zangu na mimi kuwafundisha vijana wenzangu pale biashara yangu itakaposimama,” amesema muhitimu huyo.