March 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mmoja wa wananchi akimdhibiti "kibaka" asikimbie baada ya kudaiwa kuiba ndoo ya maji kwa ajili ya kunawa mikono ili kujikinga na maambukizi ya ugonjwa wa Corona. (Picha na Suleiman Abeid, Timesmajira, Shinyanga)

Aambulia kipogo kwa kuiba ndoo ya kunawia ili kujikinga na Corona

Na Suleiman Abeid, Shinyanga

KIJANA mmoja mjini Shinyanga ambaye hakufahamika jina wala makazi yake mara moja amenusurika kufa baada ya kushambuliwa kwa kipigo na wananchi wenye hasira akituhumiwa kuiba ndoo inayotumika kwa ajili ya watu kunawa mikono kujikinga na ugonjwa wa Corona.

Kwa mujibu wa mashuhuda wa tukio hilo ambalo limetokea maeneo ya mjini kati leo saa 2.20 asubuhi, kijana huyo anadaiwa kuiba ndoo hiyo kwenye moja ya vibanda vya mama Lishe maeneo ya mtaa wa Ikelenge mjini Shinyanga.

Mashuhuda hao wamefafanua kuwa, wakati akielekea maeneo ya Soko Kuu la mjini Shinyanga kwa ajili ya kutafuta mteja wa kumuuzia ndoo hiyo, mmiliki wake alibaini kuibiwa ndoo hiyo na kuanza kumfuatilia huku akiomba msaada kwa baadhi ya wananchi waliokuwa maeneo ya viwanja vya ofisi za CCM ambao walimuona na ili kujihami, alianza kukimbia akiwa na ndoo aliyoiba na kuingia ndani ya eneo la Soko Kuu la mjini Shinyanga.

Akiwa katika harakati za kujinusuru na kipigo, aliamua kukimbilia ndani ya jumba la wauzaji wa nafaka mchanganyiko ambapo alidakwa na wafanyabiashara na kulazimika kuitupa chini ndoo hiyo huku akijitetea kwa bidii kwamba yeye siyo mwizi lakini watu wenye hasira walimuadhibu kwa kipigo lakini alipopata upenyo aliwatoroka na kukimbilia mtaani.

Baada ya kukimbia, watu wenye hasira walimkimbiza huku wakimshambulia kwa kutumia mawe na fimbo lakini baadaye walipomkamata, waliamua kumpeleka kituo cha Polisi ili kunusuru asiuawe na watu hao.