May 10, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wizara ya Maliasili na Utalii yatembelea wadau wa malikale Dar

Na Mwandishi wetu

Wizara ya Maliasili na Utalii imejipanga kuhakikisha Majengo ya kale yaliyopo Jijini Dar es Salaam yanahifadhiwa kitaalam kwa kutoa muongozo wa ukarabati wa Majengo hayo.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Idara ya Malikale nchini Dkt. Christowaja Ntandu kwenye ziara yake ya kutembelea Makumbusho ya Ukombozi wa Bara la Afrika na wadau wanaomiliki Majengo ya kale Jijini Dar es Salaam wakiwemo watu/Sekta binafsi na Taasisi za Kidini kwa lengo la kujionea hali ya Majengo hayo na kupata uwelewa wa pamoja wa Uhifadhi wake.

Dkt. Ntandu ameongeza kuwa Wataalam waliopo kwenye Idara na Makumbusho ya Taifa wamejipanga kuhakikisha wanatoa miongozo ya kitaalam ya ukarabari wa Majengo hayo ya Kale katika Jiji hilo kama sehemu ya Mashirikiano na wamiliki katika Uhifadhi wake na kuyatangaza ili kuvutia Watalii wa ndani na nje katika Jiji la Dar es Salaam.

Naye Mratibu wa Kituo cha Urithi wa Ukombozi wa Bara la Afrika,Boniface Kadili, amesema Kituo hicho kitaendelea kushirikiana na Wizara ya Maliasili na Utalii katika Uhifadhi wa Historia adhimu ya mchango wa Tanzania katika Ukombozi wa Bara la Afrika na kitendo cha Wizara hiyo kutembelea wadau wa Malikale itaongeza kasi ya Uhifadhi na Utangazaji wa Vivutio vya Malikale nchini.

Akizungumzia ziara hiyo ya Mkurugenzi huyo wa Idara ya Malikale nchini, Mchungaji Kiongozi wa Kanisa kuu la Kilutheri Tanzania ( Tanzania Front) Mchungaji Charles Mzinga ameishukuru Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kuona Umuhimu wa kuwatembelea wadau kwenye maeneo yao, kusikiliza changamoto na kubadilishana uzoefu wa Uhifadhi Shirikishi wa Majengo ya Kale wanayomiliki.

Akiwa ameongozana na Wataalam kutoka Idara ya Mambo ya Kale na Makumbusho ya Taifa, Dkt. Ntandu ametembelea, Kituo cha Urithi wa Ukombozi wa Bara la Afrika, Kanisa Kuu la Lutherani la Azania Front, Mgahawa wa Cosy Cafe (City corner Restaurant), Kanisa Kuu la Katoliki la Mtakatifu Joseph, Kanisa Kuu la Kianglikana Mtakatifu Alban, Msikiti wa Wahindi Kisutu na Shule ya Kisutu zamani D A .