April 16, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wizara ya Fedha na Mipango yawataka PSPTB kusimamia maadili ya wataalamu wa ununuzi na ugavi

Na Zena Mohamed,TimesMajiraonline,Dodoma.

WIZARA ya Fedha na Mipango imesema kupitia vyombo vya habari na kaguzi mbalimbali bado zinaonyesha kuna wataalam wa ununuzi na ugavi wanakiuka maadili ya taaluma yao.

Kutokana na hayo imetoa maelekezo kwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya wataalam wa  ununuzi na ugavi na
wajumbe wake kuchukua hatua za kinidhamu kwa wanaokiuka maadili ya taaluma kwa kuzingatia miiko na maadili ya taaluma ili kuweza kuongeza nidhamu katika taaluma hiyo.

Hayo yamesemwa jijini hapa leo na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango,Lawrence Mafuru kwa niaba ya Waziri wa Wizara hiyo Dkt.Mwigulu Nchemba  katika halfa fupi ya uzinduzi wa Bodi ya Wakurugenzi ya bodi ya wataalam wa ununuzi na ugavi(PSPTB),ambapo ametoa  wito kwa bodi hiyo kwenda  kusimamia kwa ukamilifua Sheria waliyoianzisha wenyewe,

“Naomba mtambue kuwa wadau wa ununuzi na ugavi wana matumaini makubwa kutoka kwenu kwani nyie ndio mtatoa dira ya chanya katika kutekeleza majuku yao na hii inajumuisha usimamizi wa maadili na mienendo ya Wataalam, uhuwishwaji na utengenezaji wa mitaala unaozingatia umahili wa kitaaluma na mahitaji ya soko, uandaaji na usimamiaji wa miongozo mbalimbali inayohusu taaluma, kufanya tafiti mbalimbali zinazohusu taaluma na kutoa majibu kwa changamoto zinazojitokeza kwenye taaluma, utoaji wa mafunzo endelevu kwa wataalam na wadau wengine kwenye mnyororo wa ununuzi na ugavi ili kuongeza tija katika utendaji, kufanya kazi za ushauri zinazohusu taaluma ya ununuzi na ugavi na kusimamia vyema matumizi ya tehama na mifumo ya kielectroniki katika shughuli za kusajili wa wataalam,”amesema.

Aidha amewahakikishia kuwa serikali kupitia Wizara hiyo itawapa ushirikiano kwa hatua zinazolenga kuondoa kabisa uzembe na ukiukwaji wa maadili katika fani ya ununuzi na ugavi kwani pesa nyingi za serikali, zinatumika kupitia taaluma hiyo.

Pia niwaombe kuhakikisha waajiri wote wanatoa ushirikiano kwa Bodi hii, haswa linapokuja suala la usimamizi wa maadili kwa wataalam waliosajiliwa na Bodi.

“Waajiri wanaaswa kutoa taarifa kwenye Bodi zinazohusiana na ukiukwaji wa maadili kwa wataalam, ili hatua stahiki ziweze kuchukuliwa kwani hakuna ufanisi bila maadili na weledi na mhakikishe waajiri wote wanaajiri watumishi wenye sifa stahiki zinazotambuliwa na sharia ya PSPTB na kuzingatia mahitaji yaliyopo kwenye Waraka wa Maendeleo ya Utumishi Na. 3 wa mwaka 2015 wa kada zilizopo chini ya Wizara ya Fedha na Mipango,

“Wizara yangu itaendelea kuisaidia Bodi  ili iweze kutekeleza majukumu yake kama ulivyoanisha kwenye hotuba yako napenda kusisitiza usimamizi mzuri wa rasilimali watu pamoja na matumizi sahihi ya rasilimali fedha ili malengo yaliyopangwa na PSPTB yaweze kutekelezwa kwa ufanisi,”amesema.

Hata hivyo amewasisitiza kuhakikisha kuwa wafanyakazi wanafanya kazi katika mazingira yenye utulivu wa kutosha ili waweze kutoa tija katika utendaji wao.

Kwa upande wake  Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya PSPTB,Jacob Kibona ameeleza kuwa Bodi ya Wataalam wa Ununuzi na Ugavi, imepewa jukumu la kusimamia misingi ya taaluma ya ununuzi na ugavi na mienendo ya wataalamu wake.

Pia amesema Bodi inawajibu wa kuzalisha wataalam wenye weledi na uwezo wa kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia maadili na miiko ya taaluma yao hivyo
amegaidi kuwa Bodi yake itasimamia na kuimarisha taaluma ya ununuzi na ugavi sambamba na kuongeza nguvu ya kupambana na vitendo vyote vinavyokinzana na maadili ya kitaaluma ya ununuzi na ugavi kama ubadhirifu wa mali, rushwa na ukiukwaji wa taratibu za ununuzi na ugavi.

“Hili litakuwa ni kipaumbele kwa Bodi yangu ili tuweze kuwa na wataalam waadilifu wanaosimamia zaidi ya asilimia 70 ya bajeti ya Serikali inayoelekezwa kwenye manunuzi,”amesema Kibona.