April 27, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mkuu wa TAKUKURU mkoani Dodoma Sostenes Kibwengo akiongea na waandishi wa habari(hawapo pichani).

Kampeni ‘ULIPO TWAJA’kuelimisha wananchi kubaini viashiria vya rushwa na ubadhirifu yaanzishwa TAKUKURU Dodoma

Na Joyce Kasiki,Timesmajira online,Dodoma

TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU)mkoa wa Dodoma imeanzisha kampeni ya ‘ULIPO TWAJA’yenye lengo la kuwafuata wananchi mahali walipo katika maeneo ya mikusanyo ili kuwapa elimu kuhusu rushwa na ubadhirifu ili kuwa na uwezowa kubaini viashiria vya vitendo vya rushwa na ubadhirifu wa miradi ya maendeleo na kuitolea taarifa katika vyombo vinavyohusika.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jijini Dodoma,Mkuu wa TAKUKURU mkoa wa Dodoma Sostenes Kibwengo amesema kuwa wameamua kuanzisha kampeni hiyo ili kuyafikia makundi ya watu wengi kwa wakati mmoja huku wanakofanya shughuli zao bila kuziathiri.

“Unajua tukiitisha mikutano siyo rahisi mtu kuacha shughuli zake akaenda mkutanoni,ndio maana sisi tumeamua kuanzisha kampeni hii kwa maana kwamba tutawafuata wananchi huko iwe kwenye mikusanyiko,sokoni,kwenyue kahawa na mahali pengin pengi lengo ni kuhakikisha ujembe unafika kwa wananchi wengi kwa kuwafuata waliko.”amesema Kibwengo

Kibwengo amesema,hadi  sasa wananchi takribani 45,000 wameelimishwa kwenye mikusanyiko 88 ndani ya mkoa wa Dodoma .

Amesema mkoa wa Dodoma unakadiriwa kuwa na wakazi 2,729,153 na kwamujibu wa sensa ya watu na makazi ya mwaka 2012 asilimia 52.2 ya watanzania ni wale wa rika la miaka 15 hadi 64 hivyo katika kampeni hiyo ya ULIPO TWAJA Takukuru Mkoa wa Dodoma imekusudia kuwafikia angalau asilimia 10 ya wananchi wa rika hilo ambao ni takribani wakazi 142,461.

Kibwengo amesema Rais wa awamu ya sita Samia Suluhu Hassan amekuwa akisisitiza umuhimu wa kuzuia na kupambana na ubadhilifu wa mali za umma badala ya kusubiri hadi zifujwe ndipo uchunguzi ufanyike .

Kwa mujibu wa Kibwengo , wao kama Taasisi ya kuzuia na kupamabana na rushwa wameona uelimishaji huo ni sahihi kwani utawafikia wananchi wanatumia muda mwingi katika shughuli za kujipatia riziki zao masokoni,Vituo vya bajaji na bodaboda vijiwe vya kahawa au wale ambao wanaenda kupata huduma kama mikusanyiko ya wanufaika wa TASAF, siku za lishe kwenye Vituo vya afya, siku za kliniki au chanjo,stendi za daladala na mabasi.

“Lengo la kampeni hii ni kuwafikia wananchi ambao kulingana na aina ya kazi au Biashara wanazofanya sio rahisi kuwapata kwenye mikutano ya hadhara au mikutano mingine rasmi kama ya Vijiji na Mitaa inafahamika wazi wengine uendeshaji wa maisha yao hutegemea uwepo wao katika maeneo hayo yamikusanyiko hivyo sio rahisi kuondoka na kuacha shughuli zao ili wahudhurie mikutano ya hadhara ,”amesema Kibwengo.

Aidha amesema  iwapo mkusanyiko husika utakuwepo saa 12 asubuhi  basi ULIPO TWAJA itawafuata na kuwaelimisha hata kama mkusanyiko  huo utakuwa mchana au njioni .