May 8, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

PBWB yawaonya wanaotirirsha majitaka eneo la Bomba mbuzi

Na Mwandishi wetu, TimesMajira Online

Tayari PBWB imechukua sampuli ya Maji katika mto Karanga Manispaa ya Moshi, kufuatia kutiririka kwa maji taka na yale ya kiwanda bia cha Serengeti Mjini hapa.

Mkurugenzi wa PBWB mhandisi Segule Segule amesema mto huo umepokea maji hayo kwa Takribani wiki mbili baada ya mfumo wa maji taka unaosimamiwa na mamlaka ya majisafi na usafi wa mazingira Mjini Moshi (Muwsa) kuziba kutokana na watu wasiojulikana kutupa taka ngumu.

Segule amesema hata hivyo mpaka sasa hakuna athari za kiafya zilizoripotiwa kwa kuwa maji ya mto huo hayatumiki kwa ajili ya kunywa wala kupikia Bali shughuli za Kilimo na matumizi mengine.

“Tumechukua sampuli hii ili kujiridhisha kama hakuna athari za kimazingira na kama zipo na kwa kiwango gani yanaweza kuendelea kutumika ama la…. ama Yana athari kiafya”alisema

Alisema kazi ya kusafisha mfumo huo inafanywa kwa ushirikiano baina ya Pangani, Muwsa pamoja na Mamlaka ya Maji Arusha ambayo imetoa mitambo maalumu ya kusafisha mfumo wa maji taka.

Mhandisi Segule alisema katika hatua za awali wananchi wa mitaa ya Bomambuzi walipata adha ya kutiririkiwa na maji taka na kuleta na tishio la kuwapo kwa magonjwa ya mlipuko sanjari na uchafuzi wa mazingira.

Alisema pamoja na utaratibu unafanyika sasa wa kusafisha mfumo huo pia bodi itafuatilia ili kuona maeneo halisi yaliyotupa taka ngumu ili wachukuliwe hatua za kisheria.

Kwa upande wao wakazi wa Mtaa wa Bomambuzi, Magdalena Mushi na Sofia Msangi walisema maji hayo yalileta taharuki kubwa kwani watoto walikuwa wakichezea.

Naye Diwani wa viti maalumu kata ya Bomambuzi,Faidha Hemed alitaka wananchi kuheshimu miundombinu ya maji taka kwani baada ya kuharibika wanaoathirika ni wao kabla ya matengenezo kufanyika.

Mkurugenzi wa bodi ya Maji bonde la Pangani (PBWB) mhandisi Segule Segule(katikati) akifafanua jambo mbele ya baadhi ya watumishi wa bonde Hilo pamoja na Mamlaka ya Maji safi na usafi wa mazingira Mjini Moshi (Muwsa) kuhusu kuziba kwa mtandao wa maji taka katika kiwanda cha bia cha Serengeti Mjini hapa.