May 8, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

TRA yahimizwa kuongeza zaidi makusanyo mapato ya ndani,yapongezwa kwa ukusanyaji wa sasa

Na Joyce Kasiki,Timesmajira online,Dodoma
NAIBU Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango Lawrence Mafuru amewataka watumishi wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Kutathimini namna wanavyoweza kuishauri Serikali katika suala zima la ukuaji wa uchumi kwani ushauri wao unabeba  maslahi mapana ya Taifa na kuzingatia vipaumbele vya Serikali ya awamu ya Sita .
Mafuru ameyasema hayo wakati akizundua Baraza jipya la wafanyakazi wa Mamlaka hiyo ambalo limeundwa kwa mara ya kwanza tangu kuanzishwa kwa Mamlaka hiyo mwaka 1996/97 huku akisema,anakaribisha mawazo ya wadau hasa  watumishi wa TRA ili waweze kusadiana kutunga sera na sheria zitakazopelekea kuongezeka kwa mapato ya ndani.
Aliwataka wajumbe wa Baraza hilo waliochaguliwa kutumia nafasi waliyoipata katika kuwaunganisha  watumishi na viongozi wa ofisi ili waonyeshe imani yao kwa watumishi hao.
“Ni imani yangu kuwa ushiriki wenu kwenye baraza hili utakuwa na tija na utawezesha Baraza hili kutoa mchango katika maendeleo ya Mamlaka yetu”alisisitiza
Kuhusu majukumu ya TRA                                                   
Alisema majukumu ya msingi ya TRA ni kukadiria ,kukusanya na kuhasibu mapato ya serikali kutokana na sheria za kodi ,kuhimiza uwajibikaji wa hiari miongoni mwa walipa kodi na kuishauri serikali kuhusu Sera na taratibu za kodi na mfumo wa usimamizi wake huku akiwataka kutimiza majukumu hayo kikamilifu kwa maslahi mapana ya Taifa.
“Baraza hili lina wajibu wa kuwa chombo cha kufanya tathimini ya jinsi gani majukumu haya yanatekelezwa kwa ufanisi …,watumishi acheni  kufanya kazi  kufanya kazi kwa mazoea na kuhakikisha utendaji wenu  unaleta tija katika serikali.”
Aidha amewataka kuwa na data na taarifa za kuaminika kwani ndio msingi wa ukuaji wa uchumi.
“Data ndio injini ya ukuaji wa uchumi,uwe unafanya biashara,uwe unatunga sera…, hakuna namna utatunga sera sahihi,utaweka mikakati ya biashara kama huna data na taarifa za kuaminika,ni muhimu kuwekeza kwenye eneo hilo ili tunapotiunga sera za uchumi tuwe tunazitunga huku tukiwa tumejiridhisha kwamba matokeo ya sera hizo yatakuwa yale yaliyotarajiwa yanayotokana na data.”alisema na kuongeza kuwa
“Kwa hiyo endeleeni kufanya jitihada za kuboresha eneo hilo kwa kuwa ni eneo la muhimu sana katika kuongeza wigo wa ukusanyaji kodi ,kumekuwa na jitihada kwa kutumia vyanzo vipya vya mapato na kwa kutumia ushauri ambao tumekuwa tukiupata kutoka TRA…, hivi sasa tunaendelea na zoezi la kupokea maoni kutoka kwa wadau namna ambavyo ‘shedual’ ya kodi itakavyokuwa katika mwaka ujao wa fedha ,
“Hivi karibuni tutaingia kwenye mzunguko wa bajeti ya 2022/23 na mjadala mkubwa utakuwa ni vyanzo vipya vya mapato ,tutategemea sana utendaji wenu katika kufanikisha ajenda ya maendeleo ni kubwa na serikali inataka ilete maendeleo kwa haraka kwa sababu fursa zilizopo kwenye nchi zetu za ukanda wa Afrika Mashariki na bara la Afrika na dunia kwa ujumla ni nyingi ,
“Lakini fursa hizo zinaweza tu kuwa real kwetu sisi ikiwa kama tutajipanga vizuri,tunatakiwa kuboresha miundombinu yetu ya usafiri,kuboresha mazingira yetu ya ufanyaji biashara,kuvutia mitaji kutoka nje ,yote haya yatafanikiwa ikiwa tutakuwa na sera za kodi zinazochochea ukuaji wa uchumi na hivyo basi tutaweza kuwa na nchi yenye uchumi shindani na hivyo kuleta maendeleo ambayo tunayatarajia kwenye nchi yetu na kupunguza umasikini ule ambao tunalenga kuupunguza ifikapo mwaka 2024/2025 .”
Mafuru alisema, lengo ni kuhakikisha pato la kila mtanzania linakuwa la wastani wa dola 3000 hukua kisema,ili suala hilo lifanikiwe ni kuwa na uwezo wa   kupata mafanikio makubwa katika kuwezesha upatikanaji wa mapato ambayo yatachangia sekta nyingine za kiuchumi.
Aidha ameipongeza Mamlaka hiyo kwa ukusanyaji mzuri wa mapato huku akisema kuna jambo la kujivunia katika eneo hilo na kuwataka waendelee kujiwekea malengo ya ukusanyaji kodi na kuyafikia.
Awali  Kamishna Mkuu wa TRA Alphayo Kidata ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza jipya la TRA amesema Mamlaka hiyo imefikia wastani wa makusanyo ya shilingi trilioni 1.85 hivi sasa kutoka shilingi bilioni 42 kwa mwaka katika kipindi cha mwaka 1996/97 wakati mamlaka hiyo ilipoanzishwa.
Naye Kamishna wa Kazi Ofisi ya Waziri Mkuu.Kazi,Ajira,Vijana na Watu wenye Ulemavu Suzan Mgangwa ameipongea Mamlaka hiyo kuhusu Baraza hilo linalowaweka pamoja wawakishi na watumishi wa TRA kote nchini ili kufanya majadiliano kuhusu utekelezaji wa Mipango ya Mamlaka kwa lengo la kuongeza tija na ufanisi sehemu za kazi.