May 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Serikali yavunja kamati ya urasimishaji Zenze, kuundwa tume kuchunguza malalamiko

Judith Ferdinand, TimesMajira Online, Mwanza

 Waziri wa Ardhi,Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mbunge wa Jimbo la Ilemela Dkt.Angeline Mabula amevunja kamati ya urasimishaji wa ardhi ya mtaa wa Zenze Kata ya Kiseke kufuatia uwepo wa malalamiko kutoka kwa wananchi juu ya uuzaji wa ardhi za wananchi .

Ambapo katika tuhuma hizo mmoja wa watuhumiwa wanahusika na uuzaji wa ardhi za wananchi hao kinyume na utaratibu ni pamoja na Mwenyekiti wa Mtaa huo.

Dkt.Angeline amatoa maamuzi hayo mara baada ya kupokea malalamiko kutoka kwa wananchi katika mkutano wake wa kusikiliza kero, changamoto pamoja na kukagua utekelezaji wa miradi ya  maendeleo Jimbo humo, uliofanyika shule ya sekondari Angeline Mabula iliopo Kata ya Kiseke.

 “Mtaa wa Zenze kumekuwa na malalamiko mengi juu ya ardhi hususani ule mradi ambao ulikuwa wa Mkuu wa Mkoa ambao ndio umeleta changamoto kubwa,Ofisa Tarafa Mzava unaye mwakilisha Mkuu wa Wilaya,kwanzia sasa mimi kama Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi kamati ya ardhi ile iliokuwa ya urasimishaji katika mtaa huu,ukomo wao ni leo na wasiendelee na kazi hiyo wasimame na wasifanye kazi hiyo tena,hilo la kwanza,”ameeleza Dkt.Angeline.

Katika suala la pili amemtaka Mkuu wa Wilaya hiyo kuunda tume ambayo itapitia zoezi la urasimishaji uliofanyika katika mtaa huo wa Zenze ambapo itapewa muda wa mwezi mmoja.

“La pili nataka Mkuu wa Wilaya iundwe tume itakayo kuwa na wataalamu wa ardhi,tunawapa mwezi mmoja wapitie zoezi lote la urasimishaji wa ardhi lililofanyika hapa mtaa wa Zenze na kuangalia uhalisia,waitishe vikao na waangalie zile miniti zilizopo makubaliano waliokuwa wamekubaliana mpaka wanaenda site tujue nani anasema kweli sababu ukienda changamoto za Zenze ni nyingi kupita maelekezo,”ameeleza Dkt.Angeline.

Aidha ameeleza kuwa Mwenyekiti wa eneo hilo awe mmoja wa wale watakao husika kuhojiwa na kamati hiyo kwa sababu ndio anaye tuhumiwa kati ya  wale ambao wamefanya kazi hiyo ambayo imetufikisha hapa tulipo.

“Na katika hili niwaombe wananchi mtoe ushirikiano kwa sababu malalamiko mmeyatoa tume itakapokuja toeni ushirikiano ili tuweze kubaini nani anasema ukweli ni nani kaonewa nani hajaonewa,”ameeleza Dkt.Angeline na kuongeza kuwa

“Na kwa zile fidia ambazo mnadai na hamjalipwa tunatambua kuwa fidia ni haki yako,wewe ambaye umepewa barua ukaambiwa eneo lako hawalihitaji tena wewe endelea na kazi zako katika eneo hilo wakilihitaji tena uthamini ule wa mwanzo unakuwa umekufa,watakuja waanze  upya kwa hali halisi iliopo sasa,”.

Pia amewahimiza wananchi kuhakikisha wanapata hati kwani kupimiwa tu hakumfanyi mtu kuwa salama kati sekta ya ardhi pamoja na kuwataka wananchi kutofanya ujenzi wowote au shughuli ya uendelezaji wa ardhi bila ya kupata kibali ili kuepuka hasara ya kubomolewa nyumba zao.

“Manispaa ya Ilemela na Jiji la Mwanza,wana mpango kabambe(master plan)ambayo inaendelea mji huu hizo nyumba mnazo jenga bila utaratibu mtavunjiwa mtakula hasara,ni waombe msijenge nyumba yoyote bila kupata kibali cha ujenzi,usifanye lolote la uendelezaji kwenye ardhi yako bila kupata kibali,na wale  ambao wamerasimishiwa bado pengine hawajachukua hati zao,kurasimishiwa ukawekewa vingingi pekee yake kwako havina salama katika sekta ya ardhi na ndiyo hiyo inasababisha ugomvi usalama wako ni kuhakikisha umepata hati yako,utajua jirani yako ni nani mliye pakana,bikoni zako mtazijua kwa namba ukiwa na katatasi yako ndani,”.

Awali akitoa malalamiko yake mbele ya Waziri huyo,mmoja wa wananchi wa mtaa wa Zenze,Ziripa Ndaki ametoa malalamiko juu ya wizi wa viwanja ambao mmoja wa wanaotuhumiwa kuhusika na uuzaji wa viwanja hivyo ni Mwenyekiti wa mtaa huo.

“Nilimfuata Mwenyekiti wa Mtaa na kumueleza kuacha kufanya hivyo lakini hakunisikia wanakuja watu wanapaki magari huko chini wanauza ardhi wanaondoka na wanaowauzia wanawaambia kwamba una ela ya kulipia hati kama anayo anauziwa ardhi na hati anafanyiwa ‘shashaa’,pia kuna kesi iliomfunga Mwenyekiti ipo hapa,” na kuongeza kuwa

“Hapa matatizo ni mengi mpaka mimi nimeitwa chizi huku mimi ndio naangalia haya mambo watu wameuziwa ardhi zao,ardhi zinauzwa mimi naangalia nifiche sifichi ugonjwa na Mungu anisamehe ata ukiangalia humu utaona mambo mtaa wetu ulivyofanywa na wanakuchafulia jina wewe,”.

Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya,Ofisa Tarafa wa Wilaya ya Ilemela Godfrey Mzava, ameeleza kuwa kama Mwenyekiti wa Mtaa ameshitakiwa na mahakama ikamkuta na hatia ikamla jukumu, Mkurugenzi ambaye ndiye unasimamia masuala ya Utawala  na utumishi.

“Ofisa Mtendaji andika barua kwenda kwa Mkurugenzi ili Mkurugenzi kwa kushirikiana na Ofisa utumishi pamoja na mwanasheria wa Manispaa pitieni hiyo hukumu muone inasema nini mumuandikie Mkuu wa Wilaya tuje tutangaze hapa kama amekosa sifa za kuendelea kuwa Mwenyekiti wa serikali ya mtaa hatupishe ili tuweke mtu mwingine ambaye atakuwa tayari kuwahudumia wananchi mpaka mwakani tutakapo ingia kwenye uchaguzi,”ameeleza Mzava.