May 5, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wazazi waaswa kuungana na Serikali kulinda maadili

Na Penina Malundo,Dar es Salaam

DIWANI wa Kata ya Ukonga ,Ramadhani Bendera amewataka wazazi kuhakikisha wanaunga mkono jitihada za serikali katika kuboresha huduma za malezi kwa watoto wao ili kuweza kuzuia tabia zisizofaha zinazotokana na makundi rika.

Ameyasema hayo mwishoni mwa wiki katika mahafali ya 17 ya wanafunzi wa kidato cha nne katika shule huria ya Ukonga Skillfull,alisema wao kama serikali wanajitahidi sana kutengeneza mazingira mazuri na bora kwa watoto ili kuondoa au kuzimaliza kabisa tabiaz zitokanazo na makundi rika.

Amesema licha ya serikali kufanya jitihada za kuziondoa tabia hizo ni vema wazazi wakatambua kuwa tabia hizi zinazapaswa kuondolea kuanzia majumbani mwao hadi shuleni wanasoma.

”Kuna tabia nyingi chafu zinazofanywa na watoto hali hii imetufanya sisi kama Kata kuja na wazo la kutegeneza kamati ambayo inashughulika na changamoto za watoto katika shule zote zilizopo katika kata yetu ambapo kamati hiyo itakuwa inasimamiwa chini ya mtendaji kata itakayoanza kupita mashuleni,”amesema na kuongeza

”Sasa sisi tukiwa tunahudumia mashuleni ,wazazi tunaomba muhakikishe mnahudumia majumbani mwenu hapo ndipo itasaidia sisi kwa pamoja kushirikiana katika kumlea mtoto mzuri.
”leo hii msione mie nimefika hapa mkajua nimekurupuka tu ,nimelelewa vizuri na jamii ya wanaukonga ambapo ndipo ninapoishi na nilipozaliwa,hivyo mtoto alelewi na mzazi pekee yake bali na jamii inayomzunguka ,”amesema.

Kwa Upande wake Muasisi wa shule huria ya Ukonga Skillfull,Diodorus Tabora amesema mahafali hayo ni ya 17 tangu shule hiyo kuanzishwa kwako ambapo takribani wanafunzi 200 wanatarajia kufanya mitihani ya taifa ya kidato cha nne .

Amesema shule yao imejikita katika nguzo tatu ikiwemo kuhakikisha wanafunzi wanamjua Mungu na kuwa na hofu ya Mungu,Ufundishaji wa weledi pamoja na kuhakikisha wanafunzi wanakuwa na Nidhamu.

”Wazazi na walezi niwaombe kuacha kuwakatia tamaa watoto hawa ambao wamefeli kisato cha nne na kuja kurudia mtihani wanapaswa kuwasaidia katika kuwapa ushauri ambao wanaweza kurudia mitihani yao na kuweza kupata alama za juu kabisa,”amesema.

Amesema miaka ya sasa wazazi na walezi wengi wamekuwa wakiwadekeza watoto wao maisha hali inayowafanya watoto kutokuwa wakakamavu kama miaka ya nyuma.

Amesema suala la maadili sasa hivi limekuwa janga kubwa kimataifa hivyo ni lazima wapigane nayo kuhakikisha wanawalinda watoto wao katika maadili yaliyomema na mazuri ambayo yatakuja kuwaletea tija miaka ya baadae wanapokuwa wakubwa.

”Wazazi muache kuwadekeza vijana wenu,mkae nao na kuhakikisha mnawalea katika maadili yaliyomema muache kuwadekeza kwani vijana wa sasa wanaishi maisha feki ,mzazi au mlezi usimshindwe mtoto wako unapaswa kumwambia ukweli,”amesema na kuongeza

”Tujitahidi kuwalea watoto wetu katika misingi mizuri,kwani hata hizi tabia zinazotoka huko nchi nyingine na kuingia nchini ndo hizi zinazowaharibu watoto wetu,”amesisitiza.

Amesema wazazi wengi wameshindwa kufanya jukumu la malezi kwa kutokuwa karibu na watoto wao, wengi wakikimbizana na jukumu la kutafuta fedha jambo ambalo wakati fulani linawapa wakati mgumu walimu kuwa karibu na watoto kama walivyo wazazi.

“Ni muhimu wazazi kutumia muda mwingi kuwa karibu na watoto wao, mnapowapeleka shuleni zingatie kuwafatilia kila hatua yanayopitia hiyo itasaidia hata katika ufahulu wao, tumieni muda huo kuwaonyedha pia uhalisia wa maisha jinsi ulivyo, wasijaribu kuishi maisha ya mitandaoni yaani fake life ambayo kwa sasa ndiyo yanawatesa vijana wengi nchini,” amesema.