May 3, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

TTCL yatekeleza agizo la Rais

Na Mwandishi Wetu

SHIRIKA la Mawasiliano Tanzania (TTCL) limetekeleza agizo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan la kutaka uwanja wa Benjamin Mkapa uwekewe huduma ya Mtandao yaani Inteneti ikiwa ni sehemu ya ukarabati katika uwanja huo.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa huduma hiyo ya Mtandao katika uwanja huo Novemba 5,2023 Waziri wa Habari,Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Nape Nnauye amesema kutekelezwa kwa agizo hilo la Dkt.Samia linakwenda kuwasaidia mashabiki wote wanaoingia kutazama mpira kufurahia kwa kutumia mtandao wenye kasi zaidi.

“Leo tunaanza kuzindua huduma hii ya mtandao wenye kasi katika Uwanja huu wa Mkapa na kwa maagizo ya Rais Samia ni kwamba viwanja vyote vipate huduma ya mtandao ili wanaohudhuria viwanjani wafurahie Mtandao,” amesema Nape

Katika hatua nyingine Mhe.Nape amelipongeza Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL) chini ya Mkurugenzi wake Mhandisi Peter Ulanga kwa kufanikisha uwekaji wa huduma hiyo katika uwanja wa Benjamin Mkapa.

“Pigeni makofi ya kutosha kwa TTCL kwa kufanikisha hili la kuweka huduma hii ktaika uwanja huu na naamini kiwanja hiki ni cha kwanza na viwanja vingine vitafuata sasa mnawafanya mashabiki wafurahie kuja uwanjani kwa sababu wanafurahia huduma ya mtandao ambao nimefanyia majaribio na una kasi kwelikweli,”amesema Nape

Nape ameipongeza Azam Media wa kuendelea kurusha matangazo ya mpira kwa ubora huku akiamini kuwa uwepo wa Mtandao wa uhakika kutoka TTCL itaendelea kunogesha matangazo yao.