May 18, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Watuhumiwa 23 wa dawa za kulevya wapandishwa kizimbani

Na Agnes Alcardo, Timesmajira Online. Dar

Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya nchini (DCEA) kwa kushirikiana na Ofisi ya Taifa ya Mashitaka (NPS) wamewafikisha katika Mahakama ya Wilaya ya Kahama mkoani Shinyanga Watu 23 wanaotuhumiwa kujihusisha na biashara ya dawa za kulevya.

Washitakiwa wamefikishwa mbele ya Mahakama hiyo kujibu tuhuma za kujihusisha na biashara ya dawa za kulevya aina ya bangi, heroin na mirungi kinyume cha Sheria ya kudhibiti na kupambana na dawa za kulevya Sura 95 marejeo ya mwaka 2019 kifungu cha 15 A Kifungu kidogo (1) (2) na kifungu cha 17.
Akisoma Mashauri hayo 18 ya Jinai leo tarehe 12 Machi, 2024 mbele ya Hakimu Mkazi wa Mahakama hiyo Christina Chovenye, wakili wa Serikali John Hamenya alisema kuwa watuhumiwa hao walitenda makosa hayo kwa nyakati tofauti katika mwezi Februari na Machi mwaka 2023 katika wilaya ya Kahama huku wakijua wazi kuwa biashara hiyo ni kosa kisheria.

Hamenya amewataja watuhumiwa hao 23 ambao wamefikishwa mahakamani kuwa ni, Juma Lusangija (54), Mwajuma kavula(36), Tayson Mwita Marwa (23) Emmanuel Christopher (33), Amos Augustino 34, wakazi wa mtaa wa Mwime na Fred Bichuka(37) , Rojasi Daudi (18) wakazi wa mtaa wa Mhungula na Juma Merengo Merena (44) mkazi wa Kidete , Hassan ally Ngwenyau (27) mkazi wa Nyakato na Gerald Emmanuel (18) mkazi wa Nyasubi.
Wengine ni pamoja na Paulo Charles Wilson (25) Nyakato, Joseph Lugenzi, Zamoyoni Andrea (26) mkazi wa Nyashimbi , Kobelo Ntahondi(42) Mkazi wa Bukondamoyo, Raphael Masanja (37) mkazi Nyakato na Said Kayoka kayoka (27) mkazi wa Mhungula, Saidi mselem (22) mkazi wa Majengo, na Haitham salum Suleiman (31) mkazi wa Nyasubi.

Samwel Edward John (31) mkazi wa Malunga, Joseph Mussa lugenzi,(40) mkazi wa Malunga, Robert Elias Lameck (24) mkazi wa Mwitongo , Hillary salum nassoro(39) mkazi wa Malunga ,Richard Raphael mushi (30) mkazi wa Majengo, Izdory Nemes temba(23) mkazi wa Malunga, Kassim hamad amori(27) mkazi wa Nyasubi.

Watuhumiwa wote kwa pamoja wamekana mashtaka yanayowakabili na mashauri yao yameahirishwa hadi Machi 14,15 na 26 mwaka huu kwa hatua ya kutajwa na kusikilizwa baada ya upelelezi kukamilika.

Aidha kwa upande wake, Kaimu Mkuu wa Mashitaka ofisi ya Mashitaka Wilaya ya Kahama, Salome Ngubuni amesema, Ofisi ya Mashtaka imepokea majalada 18 kutoka Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya na wameyafanyia kazi kwa uharaka kuhakikisha watuhumiwa wanafikishwa mahakamani kwa haraka kwa mujibu wa sheria, ili kukabiliana na makosa wanayoshtakiwa nayo.

Hata hivyo, nafasi ya dhamana kwa watuhumiwa iko wazi kwa Watakaokidhi vigezo vya Mahakama.