May 3, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Watoto wenye ulemavu 17 wakabiliwa na changamoto ya viti mwendo

Na Esther Macha,Timesmajira Online, Rungwe

WANAFUNZI 17 wenye ulemavu katika Shule ya msingi mchanyiko Katumba (11) iliyopo wilayani Rungwe mkoani Mbeya wanakabiliwa na changamoto ya kutokuwa na viti mwendo pamoja na watoto wengine 15 kutokuwa na magongo ya kutembelea ambavyo vinapelekea kushindwa kumudu masomo yao vyema .

Hayo yamesemwa leo Meneja wa Taasisi ya Tulia Trust , Jackline Boaz wakati akikabidhi kiti mwendo kwa mtoto mwenye ulemavu wa shule ya mchanganyiko ya Katumba (11) aitwaye Michael Oscar ambapo mtoto huyo kwa muda mrefu alikuwa na changamoto ya Kiti mwendo ambapo ilimpelekea kumudu vema masomo yake.

Meneja huyo amesema kuwa wamefika katika shule hiyo ili kuweza kumkabidhi kiti mwendo mtoto huyo ambaye mzazi wa mtoto huyo alifika ofisi ya Mbunge wa Mbeya mjini kueleza changamoto ya kijana wake akiwa shule.

“Sisi kama Taasisi ya Tulia Trust kwasababu tunafanya kazi na jamii ikatupendeza kufika katika shule hii kumkabidhi kiti mwendo mtoto huyu , lakini baada ya kufika hapa tena tukakutana na changamoto nyingine kwa watoto wengine wenye ulemavu kama mtoto Michael kwa hiyo na sisi tunaahidi kurudi tena kuweza kuwasaidia watoto hawa na tulifanya hili kwa mara kwanza tulitoa viti mwendo kwa watoto wengine ambao walishamaliza shule na kwenda kujiendeleza mbele zaidi kielimu ,hawa wengine walioingia ni wapya tumepata changamoto zao kuna watoto 17 hawana viti mwendo na watoto wengine hawana magongo ya kutembelea na mimi naahidi kama mtendaji wa Tulia trust tutafikisha changamoto hizi kwa Mkurugenzi wetu na yatafanyiwa kazi “amesema Boaz.

Jane Kulaba ni Mama mzazi wa mtoto Michael ameshukuru msaada wa kiti hicho kutoka kwa Taasisi ya Tulia Trust na kusema kuwa mtoto wake alizaliwa akiwa mzima amekuja kupata ulemavu akiwa mkubwa akiwa darasa la Nne ikabidi arudi nyuma sababu ya kuumwa .

Kwa upande Mtoto, Michael Oscar ameshukuru msaada huo kiti mwendo kutoka kwa Mbunge wa Jimbo la Mbeya mjini nakushukuru msaada huo na kuahidi kusoma kwa bidii kwani kiti hicho kitakuwa msaada kwake tofauti na ilivyokuwa awali alipokuwa hana kiti ambapo hali hiyo ilimpelekea kuchelewa shule.

Boniface Mgina ni Mkuu wa kitengo cha watoto wenye ulemavu amesema kiti mwendo hicho kitamsaidia kuwahi darasani pamoja na kwenye bwaro la chakula nakuomba wadau wengine kuiga mfano huo wa Tulia Trust katika kuwasaidia watoto wenye ulemavu ili waweze kupata mahitaji muhimu ,nakusema si kwamba Taasisi hiyo ina fedha bali ni upendo tu walionao.

Aidha ameshukuru serikali kwa kuwasapoti katika kuwapatia walimu , vitabu vya kufundishia ,miundo mbinu kwa kujenga madarasa matano na bweni moja nakuomba serikali isiishie hapo kwani bado kuna watoto wengine wenye ulemavu bado hawajatambuliwa watazidi kuja, pia alisema kuna madarasa mengine yamechakaa serikali na wadau waliosoma wasaidie kukarabati madarasa hayo matano wakarabati ili watoto wenye ulemavu waweze kusoma vizuri na kuwa dawati moja wakikaa watoto wawili au mmoja itaweza kuwa msaada kwa watoto wenye ulemavu.

Shule ya msingi Katumba 11 ipo mkoani mbeya katika kata ya Kata ya katumba inahudumia wanafunzi mchanganyiko wakiwemo wenye ulemavu wa akili ,viungo , ngozi na kusikia pamoja na wasioona .

Picha ya pamoja Meneja Tulia Trust na mtoto Michael na mama mzazi na uongozi wa shule ya Katumba
Darasa la watoto wenye ulemavu lilojengwa kwa fedha za ndani za Halmashauri ya Wilaya ya Rungwe
Jengo la zamani ambalo uongozi wa shule umeomba likarabatiwe ili kupunguza msongamano wa wanafunzi