May 16, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Watoto wenye mahitaji maalum wapewa tabasamu

Judith Ferdinand, TimesMajira Online,Mwanza

Shirika la Plan International limewasaidia vifaa saidizi wanafunzi wenye mahitaji maalum kwa Halmasahauri ya Jiji la Mwanza na Manispaa ya Ilemela mkoani Mwanza wakiwemo wa kitengo cha watoto wenye mahaitaji maalumu kutoka shule ya msingi Igogo jijini hapa.

Huku shirika hilo likisisitiza elimu jumuishi kwa wote ikiwa ni pamoja na watoto wenye ulemavu,wa kike na kiume,ili isifike mahali watoto wenye mahitaji maalum wakaachwa.

Vifaa hivyo vyenye thamani ya milioni 21, vitawanufaisha watoto 66,vimetolewa kwa wanafunzi wa shule ya msingi Igogo ambao wamepokea viti mwendo 4,vifaa vya masikioni 5,miwani 3,pia katika shule ya msingi Buhongwa,Kayenze na shule nyingine zilizopo katika halmasahauri hizo.

Meneja wa shirika la Plan International Mkoa wa Mwanza Majani Rwahambali,akizungumza wakati wa zoezi la utoaji wa vifaa hivyo lililofanyika katika shule ya msingi Igogo,wilayani Nyamagana jijini Mwanza Aprili 25,mwaka huu, ameeleza kuwa wametoa vifaa hivyo baada ya kubaini kuwa miongoni mwa watoto hao wanashindwa kuhudhuria masomo vizuri huku wakifahamu kuwa kundi hilo lina uhitaji mkubwa wa vifaa saidizi.

Meneja wa shirika la Plan International Mkoa wa Mwanza Majani Rwahambali,akizungumza wakati wa zoezi la utoaji wa vifaa saidizi kwa watoto wenye mahitaji maalumu,vilivyotolewa na shirika hilo lililofanyika katika shule ya msingi Igogo,wilayani Nyamagana jijini Mwanza.

Ambapo wameamua kutoa vifaa hivyo baada ya kupata ushauri wa wataalamu wa kiserikali ikiwemo wa elimu na afya ndio waliowaelekeza vifaa gani vinavyohitajika kwa watoto kulingana na mahitaji baada ya kubaini wakati wa zoezi la kuwatafuta na kuwabainisha watoto hao.

“Mwaka jana tumegawa vifaa kwa watoto 70 na kwa kipindi hiki watoto watakaonufaika na vifaa hivi ni watoto 66, kwa halamshauri zote mbili za Jiji la Mwanza na Manispaa ya Ilemela,”.

Ameeleza kuwa mbali na vifaa hivyo pia wametoa vifaa kwa ajili ya kituo cha Afya Kayenze kilichopo wilayani Ilemela,lengo likiwa ni kuwasaidia vijana kupata huduma za kiafya ambazo ni rafiki kwa vijana,kuwezesha kutambua makuzi yao,waishi namna gani na wajitunze vipi.

Shirika hilo limekuwa likishiriki katika shughuli za maendeleo kwa kushirikiana na serikali na itaendeleza ushirikiano huo pamoja na jamii ambapo kwa sasa wanaendelea na ukarabati wa madarasa na ofisi mbili za walimu .katika shule ya msingi Buhongwa.

Kwa upande wake Mwalimu Mkuu wa shule ya Msingi Igogo, Anthony Nelson,ameeleza kuwa kitengo hicho cha watoto wenye mahitaji maalum kina jumla ya watoto 40 kati yao wavulana ni 23 na wasichana ni 17.

Mwalimu Mkuu wa shule ya Msingi Igogo, Anthony Nelson,akisoma taarifa ya kitengo cha watoto wenye mahitaji maalumu kilichopo katika shule,wakati wa zoezi la utoaji wa vifaa saidizi kwa watoto wenye mahitaji maalumu, vilivyotolewa na shirika la Plan International.

“Kitengo cha watoto wenye mahitaji maalum kilianzishwa rasmi Februari 2021,kikiwa na watoto wenye ulemavu wa akili 21 kati yao wavulana 11 na wasichana 10,walemavu wa viungo jumla yao kuu walikuwa 28,kwa sasa kina watoto wenye ulemavu wa akili 30 kati yao 16 wavulana na 14 wasichana,wenye uziwi na usikivu hafifu wavulana 3 na msichana 1,ulemavu wa viungo 6 ambapo wavulana 4 na wasichana 2”ameeleza Mwalimu Nelson.

Sanjari na hayo Mwalimu Nelson ameeleza kuwa miongoni mwa changamoto zinazowakabili wanafunzi wenye uhitaji maalumu kutoka shule ya msingi Igogo ni pamoja na ukosefu wa darasa la kisasa lenye maliwato ndani yake,hali hiyo husababisha watoto kwenda kujisaidia mbali na chumba chao cha kusomea.

Ukosefu wa walimu wa kike,ambapo mahitaji ni walimu watano waliopo ni watatu wa kiume hivyo wanauoungufu wa walimu wawili wa kikehali inayosababisha kushindwa kuwahudumia vizuri watoto wa kike pindi wanapojisaidia.Kukosa ushirikiano kwa baadhi ya wazazi kuwaleta Watoto wao shuleni,kwani hawaoni umuhimu wa Watoto kuja shule kila siku.

Ukosefu wa baadhi ya vifaa vya kujifunzia kama vile projecta,runinga na radio vinavyosaidia kuchangamsha ubongo wa Watoto huku baadhi ya watoto kutokana na hali duni ya mazingira na maisha ya wazazi wao hivyo kushindwa kuwaleta shuleni kila siku.

Ofisa Elimu,Elimu Maalum Awali na Msingi Halmashauri ya Jiji la Mwanza,Zakiah,akitoa maelekezo kwa mzazi,jinsi ya kutumia kiti mwendo.

Naye Ofisa Elimu,Elimu Maalum Awali na Msingi Halmashauri ya Jiji la Mwanza,Zakiah Ahmed, ameeleza kuwa serikali imekuwa ikishirikiana na mashirika mbalimbali kufanya juhudi kubwa za kutatua changamoto za kielimu kwa watoto wenye mahitaji maalumu.

Ambapo awali Halmashauri Jiji la Mwanza ni vitengo tisa tu ndio vilikuwa vinapata chakula lakini mpaka sasa ni shule 44 zenye watoto wenye mahitaji maalum vinapatiwa pesa ya chakula na serikali ikiwemo shule ya msingi Igogo ambayo imeanza kupokea fedha hizo tangu Oktoba mwaka jana inayotolewa kila mwezi zaidi ya laki tano.

Ameeleza wamepokea vifaa saidizi kwa ajili ya watoto wenye mahitaji maalumu kutoka kwenye shirika hilo ambavyo watavigawa kwenye shule mbalimbali za Mwanza Jiji.

Miongoni mwa vifaa vilivyotolewa ni viti mwendo 32,vifaa saidizi kwa ajili ya usikivu 25,magongo 2,miwani jozi 4 kwa ajili ya watoto wenye uoni hafifu,vifaa kwa ajili ya watoto wenye ulemavu wa ngozi,ambavyo vitawafikia watoto 66, hivyo watavisimamia na kuvitunza pamoja na kuhakikisha vifaa hivyo vinawafikia walengwa.

“Nakiri kupokea vifaa vyenye thamani ya milioni 21, kutoka kwa wafadhili wetu Plan International,mwaka jana walitupatia vifaa vingi na mwaka huu pia,kila mtoto anapewa kifaa kulingana na mahitaji yake baada ya wataalamu wetu kuthibitisha kuwa mtoto fulani anatakiwa kupewa kiti mwendo au fulani anatakiwa kupewa kifaa saidizi cha kusikiliza,”.

Hata hivyo baadhi ya wazazi wa watoto wenye mahitaji maalum akiwemo Meresiana Deonise, wamelishukuru shirika hilo kwa kuwasaidia vifaa hivyo kwani vitawarahisishia wakati wa kuwapelekea shule na kuwarejesha nyumbani watoto wao.