April 27, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wamuomba Rais Dkt. Samia kuunda Tume kuchunguza mgogoro wa mipaka Mirerani.

Na Mwandishi wetu, Mirerani

Wachimbaji wadogo wa Madini ya Tanzanite Mirerani ,wameomba serikali kuunda Tume kuchunguza migogoro ya mipaka baina ya migodi ya wachimbaji wadogo na mgodi wa kitalu C ambayo inamilikiwa kwa sasa na Kampuni ya Franone Mining Ltd.Kampuni hiyo ya Franone inalalamikiwa kwa kukata migodi ya wachimbaji wadogo na kuwarudisha nyuma bila kuzingatia sheria ndogo ndogo ambazo wamekuwa wakitumia baada ya kutobozana.

Kutokana na migogoro hiyo migodi mikubwa minne ambayo imetoa ajira kwa wachimbaji wadogo zaidi ya 2000 ambao Sasa wameshindwa kuendelea na uchimbaji na uzalishaji wa Madini na hivyo kukabiliwa na hali ngumu ya maisha.Migodi hiyo ni GEM& Rocks,Edward Mollel, Tanzanite Exploration Ltd ,Saniniu Laizer (Bilionea Laizer) na Mgodi wa Manga Gems(T) Ltd.Akizungumza na waandishi wa habari mchimbaji mdogo Julian Laizer kwa niaba ya wachimbaji wengine,amesema Kampuni ya Franone imekuwa ikiharibu migodi ya jirani na kuchukuwa vifaa vya uchimbaji bila kuzingatia sheria.

“Tunamuomba Rais Samia Suluhu kuunda Tume kumaliza mgogoro huu kwani kwa muda mrefu umekosa Suluhu na ambao tunapata Shida ni sisi wachimbaji wadogo kwa sababu viongozi wa Wizara ya Madini wanashindwa kutenda haki”amesema

Mchimbaji mwingine ambaye pia ni kiongozi wa chama Cha wachimbaji wadini Mererani,(MAREMA) jina linahifadhiwa amesema serikali inapaswa kuingilia kati na kuitaka Kampuni ya Franone kurejesha.zana za uchimbaji Madini za Kampuni nyingine lakini pia miundombinu.

“Kutokana na upekee wa Madini haha Duniani ni muhimu watanzania kunufaika na Madini haya kwa kukubali Madini yachimbwe kwa kufata jiolojia ya miamba yenye madini na kama Kuna changamoto sheria ndogo ndogo za migodini zitumike”amesema.

Ameshauri pia serikali kupitia upya sheria ya uchimbaji Madini ya Vito ili itofautiane na Madini mengine ambapo iondowe sheria ambayo inataka wachimbe Madini kwenda chini badala kufuata miamba hasa kwa kuzingatia eneo la Mirerani ni dogo na linategemewa na maelfu ya watu.

Amesema madini ya Tanzanite hayachimbwi kama choo bali ni kufuata miamba hivyo ni muhimu serikali kuunda Kamati kutafuta Suluhu ya kudumu badala ya kukumbatia mchimbaji mmoja.

Hivi karibuni Waziri wa Madini ,Anthony Mavunde alitembelea migodi hiyo ambapo pia wachimbaji wadogo walilalamikia mgogoro wa mipaka na kutaka Wizara kutafuta Suluhu ya kudumu.Hata hivyo Waziri Mavunde alitaka Kila mchimbaji kuchimba katika eneo lake la lesseni na sio kufuata jiolojia ya miamba ya Madini kama wachimbaji wadogo wnavyotaka.Mwisho