April 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wamachinga: Vitambulisho vimetutua mzigo

Na, Pius Ntiga, Moshi.

WAFANYABIASHARA wadogo maarufu kama Machinga katika Wilaya ya Moshi Mkoani Kilimanjaro, wamesema vitambulisho vya wajasiriamali wadogo vimewatua mzigo, hivyo wanashangaa baadhi ya Wanasiasa wanaopotisha kuhusu vitambulisho hivyo.

Wakizungumza na mwandishi wa habari hizi, anayeangazia mafanikio yaliyofikiwa na Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais John Magufuli, wafanyabiashara hao wamesema utamu wa vitambulisho hivyo wanaujua wao.

Wamesema awali walikuwa wanalipa Shilingi 500 kwa siku, sawa na shilingi 182,000 kwa mwaka, kiasi ambacho wamesema ni kikubwa ukilinganisha na shilingi 20,000 wanayolipa sasa kwa mwaka.

“Tulikua tunalipa shilingi 200 ya usafi kwa siku, sawa na shilingi 73,000 kwa mwaka, ambapo sasa mateso kama hayo hatuyapati tena tunamshukuru sana Rais Magufuli kwa kutuona na tutampa zawadi mwaka huu” wamesema baadhi ya Machinga.

Kwa mujibu wa wafanyabiashara hao, mkombozi wao ni Rais Magufuli, na kwamba amekuja na Mpango wa shilingi  20,000 tu kwa mwaka, na sasa kero za mgambo kutufukuza haipo tena.

“Nikwambie tu kuwa mabenki nayo yamesema kwa kuwa tuna vitambulisho, shughuli zao zimerasimishwa sasa, hivyo tumeanza kupewa mikopo, huku vitambulisho vikiwa ni dhamana yetu,” wameeleza

Wamesema hivi sasa hawasumbuliwi tena na askari wa jiji wala mgambo kama ilivyokuwa hapo awali.

“Vitambulisho vya wamachinga vimetusaidia sana, tunanunua kwa ridhaa yetu, hatulazimishwi”. Wamesema Machinga.

Aidha, wamefafanua kuwa uwepo wa Vitambulisho hivyo vimeaaondolea kero na kwa sasa Biashara yao imeimarika zaidi na kipato chao kimeongezeka na wamefanikiwa kununua Ardhi na kujenga Nyumba.

Kutokana na mafanikio hayo, Mkurugenzi Mtendaji wa Manispaa ya Moshi, Michael Mwandezi, amesema tangu kuanza kwa utaratibu huo zaidi ya Asilimia 70 ya Wamachinga wamepatiwa Vitambulisho katika Manispaa ya Moshi.

Mwandezi amesema fedha inayotokana na vitambulisho hivyo kuenda Hazina na kisha kurudishwa katika Manispaa kwa ajili ya kutekeleza miradi ya Maendeleo ambayo inawagusa moja kwa moja wananchi.

“Pia tumewasaidia hawa wajasiriami kuwajengea uwezo wa kimtaji ambapo sasa wanakopesheka kupitia Vitambulisho, hivyo vimewanufaisha kwa kukopa fedha Benki”. Amesema Mkurugenzi.

Hivi karibuni baadhi ya Wanasiasa wamekuwa wakipotosha kuhusu Vitambulisho hivyo vya Wamachinga kuwa haviwanufaishi na badala yake wanaibiwa, kauli ambayo Rais John Magufuli ambaye ni Mgombea wa Urais Kupitia CCM, amewataka wafanyabiashara hao kuwapuuza Wanasiasa na badala yake waunge juhudi za serikali za kuwakomboa Wamachinga.