April 25, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wakuu wa shule zinazofeli mitihani kushushwa vyeo

Na Mwandishi Wetu, Urambo

MKUU wa Mkoa wa Tabora, Dkt. Philemon Sengati, ameagiza kushushwa vyeo kwa walimu wakuu wa shule ambao zimekuwa zikifanya vibaya katika matokeo ya mitihani ya ngazi mbalimbali ya kitaifa.

Alitoa kauli hiyo jana wilayani Urambo wakati wa mkutano na viongozi na watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Urambo kwenye ziara ya kikazi.

Dkt. Sengai alisema walimu wakuu wasiokuwa wabunifu wa kuziwezesha shule zao kupandisha ufaulu wa wananfunzi ili waweze kuondokana na daraja sifuri, la nne na tatu hawafai kuendelea na nafasi zao.

Alisema ni vema wakaondolewa na nafasi zao kukabidhiwa walimu ambao wako tayari kufanyakazi kwa kujituma na uzalendo ili waweze kuchochea ufaulu katika Shule zao na Mkoa kwa ujumla.

“Tunaka walimu wale ambao wako ‘committed na willingness, na wanafanyakazi kwa uzalendo mkubwa hao ndio tuendelee kuwafanya kuwa wakuu wa shule ili waendelee kuwa injini ya ufaulu wa shule zetu,” alisema.

Dkt. Sengati alisema walimu lazima wasaidie kusimamia maadili na kuwahimiza wanafunzi kusoma kwa ushirikiano na kuwawezesha kuongeza ufaulu ili wautangaze kwa kushika nafasi za juu.

Alisema moja ya kipaumbele cha uongozi wake ni elimu kwa kuwa elimu ndio itasaidia kuwapaisha wakazi wa Mkoa wa Tabora kiuchumi na maendeleo mbalimbali.