May 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wahitimu wa kozi ya uchangaji watakiwa kuitangaza injili ya kweli

Israel Mwaisaka, TimesMajira Online, Rukwa

MAKAMO mkuu wa chuo cha Bibilia  cha AMO (African Ministries Outreach Bible College) Mhandisi Nelson Makoti amewataka wahitimu wa kozi ya uchungaji katika chuo hicho kwenda kuitangaza injili ya kweli na kuachana na injili potofu zilizoenea sasa za maji na mafuta zilizolenga kuwaibia Wananchi.

amesema kuwa hivi sasa kumeibuka injili za kitapeli na kwa kuwa wengi hawaifahamu Biblia kiundani ujikuta wakitapeliwa na kujikuta na wao wakieneza injili ambazo ni kinyume na mwenyezi Mungu.

Hivyo aliwataka wahitimu wa kozi hiyo ya uchungaji kuwa mstari mbele kuitumia elimu ya Biblia waliyoipata kwa kuitangaza injili iliyo ya kweli na kuondokana na injli za mazoea kama walivyokuwa wakihubiri huko nyuma kabla ya kupata elimu hiyo ya Biblia.

Makoti alisema kuwa Wachungaji wengi uendesha makanisa bila ya kuwa na elimu ya Biblia wakidai kuwa wamepata upako wa kiroho kutoka kwa Mungu huku wakiwadanganya  waumini wao kuwa mbona Yesu hakusoma lakini alifanya kazi ya Mungu sawa sawa na kuwa hayo ni maneno yasiyo sahihi ma kuwa yamepitwa na wakati na kuwa ili uweze kuwa mchungaji sahihi ni lazima upitie chuo.

Alisema kuwa elimu ya Theolojia ni muhimu sana kwa viongozi wa dini kwa maana ndani yake wanajifunza mambo mengi ikiwemo na uongozi na kuwataka waumini wa dini mbalimbali kuwataka Wachungaji wao wakasome ili waweze kuwangoza katika kweli na haki.

Rais wa  Wanafunzi katika chuo hicho Kadius Sangu alidai kuwa yeye amekua Mchungaji katika kanisa la EAGT kwa muda mrefu bila ya kwenda chuo na kuwa akilinganisha na sasa baada ya kupata elimu ya Theolojia amegundua kuwa alifanya mengi kinyume na misingi ya Biblia lakini sasa elimu aliyoipata imemuweka kwenye mstari sahihi.

Na aliitumia nafasi hiyo kuwataka Wachungaji wenzie ambao bado hawajapata elimu hiyo ya Theolojia waende wakajiunge na chuo hicho na kuwa elimu watakayoipata itawafanya waendane na mabadiliko ya dunia ya sasa na kuweza kuendana na wakati lakini kubwa ni kuitangaza injili ya kweli.

Fidelisi Maheke mmoja wa wahitimu wa mafunzo hayo ya Kichungaji amedai kuwa chuo hicho kimembadilisha kimtazamo na kuwa sasa yeye ataendelea na masomo ya juu kutoka stashahada aliyohitimu na kwenda kupata shahada ya Theolojia na kuwa hata katika Mithali 4:13 imeandikwa “mtafute sana elimu usimuache aende zake”

Mkuu wa wilaya Nkasi Peter Lijualikali akiwa mgeni rasmi kwenye mahafali hayo aliwataka Wachungaji kubadilika kifikra sasa na kila mmoja aende shule ili waweze kuendana na mabadiliko ya dunia kwani sasa ni waksti sahihi kwa viongozi wa dini kuwa na elimu stahiki ya Theolojia ili waweze kukabiliana na mazingira ya sasa ndani ya kanisa.

“Wakati wa kuendesha makanisa kwa mazoea sasa umepita kinachotakiwa kila mmoja anaetamani kuifanya kazi hiyo ni lazima awe na ujuzi stahiki na kuwa  ujuzi huo unapatikana katika vyuo vya Biblia na si vinginevyo.

Hayo ni mahafali ya kwanza kwa chuo   hicho cha African Ministries  outrech Bible College  toka kizinduliwe mkoani Rukwa ambapo wahitimu 20 wameweza kufuzu mafunzo ambapo kati yao 15 ni stashahada na 5 Shahada