May 5, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wafanyabishara Mkuranga, Kibiti wamsifu Samia uhuru wa kibiashara

Na Mwandishi Wetu, Mkuranga

WAFANYABISHARA wilayani Mkuranga na Kibiti, wamempongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa kutuliza dhorobu ya hali ya biashara nchini.

Wamesema kwenye wilaya hizo biashara zinafanyika kwa amani na utulivu bila usumbufu tofauti na miaka ya nyuma.

Wametoa pongezi hizo kwa nyakati tofauti kwenye mkutano kati ya wafanyabishara wa wilaya hizo na viongozi wa Jumuiya ya Wafanyabiashara (JWT) inayoendelea mkoani Pwani yenye lengo la kusikiliza na kutatua kero za wafanyabishara.

Mfanyabiashara Hassan Mbwana Kambangwa, amesema wafanyabiashara kwa asilimia kubwa wilayani humo wananufaidika sana tangu kuingia kwa utawala wa Rais Samia.

Amesema “Kimsingi namshuruku Rais Samia kwa kutuletea ugeni uliotupa fursa ya kuzungumza changamoto zinazotukabili, lakini sisi tangu kuingia kwa utawala huu wa Mama Samia tunafaidika nao kwa asilimia kubwa.”

Mfanyabiasha huyo ametolea mfano wa mambo wanayofaidika nayo kuwa ni mikopo, uhusiano mazuri na halmashauri lakini pia taasisi mbalimbali za kifedha ziko huru kuwasaidia wafanyabiashara.

Amesema serikali imezingatia suala la amani na utulivu na kwa mikoa mingi ilikua inapata changamoto nyingi lakini hapa wilaya ya Mkuranga wafanyabiashara wako huru na wanafanyabiashara bila bugudha.

“Tunamshukuru sana Rais Samia Suluhu Hassan tunafanyabiashara kwa amani lakini pia tunashukuru ujio huu wa leo umefanya tuweza kufunguka yale ambayo yako ndani ya moyo na tunaamini mtayafikisha,” Kambangwa.

Naye mfanyabishara Wilaya ya Kibiti, Salim Juma, amempongeza Rais Samia kwa kuona sekta ya wafanyabishara ni sehemu ya uchumi wa Taifa na kuamua kuungana kwa pamoja kutatua kero zao.

“Ili kuwa na ustawi tumefanikiwa kumpa Rais Samia, ambaye ameona umuhimu wetu na kutambua mchango wetu ndio maana leo viongozi mpo hapa,” amesema Juma.