May 8, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Waathirika unyanyasaji wa kijinsia watakiwa kupaza sauti zao

Na Mwandishi wetu, timesmajira

CHAMA cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania(TAMWA) kwa kushirikiana na wadau wakiwamo wa Mfuko wa Udhamini Wanawake Tanzania (WFT-T) na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU),kimewataka waathirika wa rushwa wa ngono na unyanyasaji wa kijinsia mahala pa kazi kupaza sauti zao ili wapate msaada na Haki zao nchini .

Akizungumza na waandishi habari leo jijini Dar es Salaam,Mkurugenzi Mtendaji wa TAMWA ,Rose Reuben amesema tatizo la rushwa wa ngono sio la kunyamaziwa sababu linaua ndoto na kuchelewesha malengo ya wanawake na watoto wa kike nchini.

Amesema kwa muda wa miaka mitano mfululizo TAMWA imetekeleza mradi wake wa kuchapisha habari za uchunguzi juu ya rushwa ya ngono kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wakiwemo mfuko wa udhamini wanawake Tanzania (WFT-T) ,taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa TAKUKURU na wanamtandao wa kupinga ukatili wa kijinsia nchini.

Amesema kila mwaka Novemba 25,wataanza safari ya siku 16 za kupingwa ukatili wa Kijinsia,safari hiyo inawakumbusha kuwa ukatili wa Kijinsia ni mchakato unaofanyiwa kazi Kila siku na unaohitaji wenye utashi wa Jamii kutekeleza.

“TAMWA imekuwa ikiadhimisha siku hii kwa kuungana na wadau wengine wanaopinga Ukatili wa Kijinsia na kukumbusha jamii kuwa ukatili upo katika sura nyingi na katika maeneo mengi,”amesema na kuongeza

“Kwa mwaka huu TAMWA katika kuadhimisha maadhimisho hayo ,tumewekeza kupingwa rushwa ya ngono na unyanyasaji wa kijinsia katika maeneo ya kazi na kwa taaluma yetu kupinga unyanyasaji huo katika vyumba vya habari na wanahabari ikiwamo katika shule za habari,”amesema Dkt.Rose.

Amesema kwa miaka mitano mfululizo TAMWA imetekeleza mradi wake wa kuchapisha habari za uchunguzi juu ya unyanyasaji wa kingono mahali pa kazi na Vyuo Vikuu kwa kushirikiana na wadau hao, TAKUKURU pamoja WFT -T.

Kwa Upande wake Mkurugenzi wa Mfuko wa Udhamini Wanawake Tanzania (WFT -T),Rose Marandu amesema rushwa ya ngono imekuwa ikiangusha ndoto za watu wengi ambapo inakuwa inadhalilisha na kuua.

“Waandishi wa habari mnapaswa kuendelea kupaza sauti juu ya masuala ya rushwa ya ngono hivyo kuna haja ya kuandika habari za kina hususani zile zinazotolewa na mashirika ya watetezi wa haki za binadamu,”amesema.

Naye Mchunguzi Mkuu wa PCCB,Dorothea Mrema amesema kwa mujibu wa makosa yote yaliyopo katika sheria ya kupambana na rushwa namba 11 ya Mwaka 2007 yapo makosa 24 huku kosa moja pekee ambalo lipo kifungu cha 15 ya kuhonga na kupokea ndilo halipo katika sheria ya uhujumu uchumi lakini mengine yote yapo katika uhujumu uchumi.

“Ni ukweli uhujumu uchumi adhabu yake ni kuanzia miaka 20 na kuendelea na makosa yote ikiwemo rushwa ya ngono yanahusishwa na sheria ya uhujumu uchumi,”amesema.