April 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Vituo utoaji mimba vyaonywa,Dkt.Gwajima asema serikali inavifuatilia

Na Joyce Kasiki,Timesmajira online,Dodoma

WAZIRI wa Maendeleo ya Jamii ,Jinsia,Wanawake na Makundi Maalum Dkt.Dorothy Gwajima amevitahadharisha vituo vinavyojihusisha na utoaji wa mimba huku akisema wizara yake inavifuatilia na hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi ya vituo vitakavyobainika kufanya hivyo.

Akizungumzia mafanikio ya wizara hiyo katika kipibndi cha mwaka mmoja wa Rais Samia Suluhu Hassan ,Dkt.Gwajima alisema,ni lazima serikali itachukua dhidi yao kwani kufanya hivyo ni kukatili uhai wa watoto waliotarajiwa kuzaliwa.

“Kuna taasisi fulani kazi yao ni kutoa mimba tutazifuatilia na tutachukua hatua za kisheria dhidi yao.”alisema Dkt.Gwajima

 Kuhusu mafanikio ya wizara hiyo Dkt.Gwajima alisema  ni pamoja na kuanzishwa kwa Programu Jumuishi ya Malezi,Makuzi na Maendeleo ya awali ya Mtoto(PJT-MMMAM) ambayo ni programu ya miaka mitano 2021/22-2025/26.

“Katika kuimarisha malezi na makuzi jumuishi ya watoto kama ilivyoelekezwa kwenye Ilani ya Uchaguzi Mkuu CCM Kifungu 93 (c) Serikali imeandaa Programu Jumuishi ya Taifa ya Malezi, Makuzi na Maendeleo ya Awali ya Mtoto (2021/22 – 2025/26) yenye lengo la kumlea mtoto wa umri wa miaka 0 – 8 ili kufikia utimilifu wake.”alisema Dkt.Gwajima

 Aidha, alisema Wizara hiyo  imejenga Vituo Jumuishi vya Kijamii vya Kulelea Watoto (Community-Based Early Childhood Development Centers) ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa Programu hiyo.

“Vituo hivyo vina lengo la kutoa huduma jumuishi za Malezi na Makuzi kwa watoto walio na umri kuanzia miaka 2 hadi chini ya miaka 5  kwa kuwapatia huduma jumuishi za afya, lishe, ulinzi, ujifunzaji na uchangamshi wa awali kabla ya kujiunga na darasa la awali. “alisema Dkt.Gwajima

Alisema katika kipindi cha Machi 2021 hadi Februari 2022, jumla ya Vituo vya mfano 30 vimejengwa katika Mikoa ya Dar es Salaam vituo 10  na  Dodoma 20.

Kwa mujibu wa Waziri huyo , Wizara imeendelea kusimamia uanzishaji na uendeshaji wa huduma za vituo vya kulelea watoto wachanga na watoto wadogo mchana ambapo katika kipindi cha Machi 2021 hadi Februari 2022, Wizara imesajili vituo 303 vilivyodahili watoto 6,772 (Me 3,194 na Ke 3,578).

Dkt.Gwajima alisema,vituo hivyo vinawezesha watoto kupatiwa huduma zinazochochea uchangamshi wa awali wa makuzi kimwili, kiakili, kihisia, kijamii na ukuaji wa lugha pamoja na kuwawezesha wazazi na walezi wa watoto kujihusisha na shughuli za kiuchumi wakati watoto wao wakiwa salama kituoni.

Alizungumzia kuhusu kuimarisha upatikanaji wa haki kwa watoto wanaokinzana na sheria sambamba na maelekezo ya Ilani ya Uchaguzi Mkuu CCM Kifungu 93 (i) Serikali kupitia wizara hiyoimefanya ufuatiliaji  katika magereza yaliyopo mikoa ya Rukwa, Katavi, Dar es Salaam, Morogoro na Dodoma.

“ Ufuatiliaji huu umewezesha watoto 16 kuachiwa huru kutoka Gereza Kuu la Segerea na kuwekwa chini ya uangalizi wa Maafisa Ustawi wa Jamii, Jijini Dar es Salaam…,aidha, watoto watano wametolewa Gereza Kuu la Segerea na wamehamishiwa Mahabusu ya watoto Upanga.