May 4, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Vigezo na masharti kwa watakaolipiwa mahari

Na Jackline Martin, TimesMajira Online

Mwenyekiti Taasisi ya Al-Hikma, Sheikh Nurdin Kishki amesema vijana 50 watakaolipiwa mahari ambao wapo tayari kuoa watatakiwa kufuata vigezo na masharti ambayo taasisi hiyo wameviweka.

Sheikh Kishki aliyasema hayo jana wakati akizungumza na waandishi wa Habari jijini Dar es Salaam na kusema kuwa moja ya vigezo na masharti waliyoyaweka kwa vijana hao ni lazima muoaji awe amefanya usajili na kujaza fomu ya maoni ambayo itapatikana kuanzia Aprili 13 – Mei 2 mwaka huu.

“Awe amefanya usaili, tutafanya usaili na kufaulu usaili wetu, lazima tuwafanyie mahojiano ili tusitupe gharama zetu kwa mtu ambaye si sahihi”.

Aidha Sheikh Kishki alisema muoaji lazima awe muislam hii ni kwasababu Mufti Mkuu ndiye anatarajiwa kusimamia ndoa hizo.

“Tunafahamu tanzania tuna dini mbalimbali hivyo akijitokeza mtu ambaye siyo muislam vipi ndoa ile itafungishwa na mufti kwa imani ya kiislam wakati yeye anaimani yake”

Pia alisema sharti lingine ni lazima muoaji asiwe na mke.

“Hii haina maana ya kwamba tunapiga vita ndoa ya wake wengi , katika uislamu hili ni sheria, katija sura ya 4:2 imetaja, lakini tunasema mwenye mke mmoja si haba kuliki yuke aliye bachela ambaye hali yake ni mbaya sana”

Sheikh Kishki alisema muoaji ni lazima awe ameshaposa.

“kuna mamia ya vijana wa kiislam wa kitanzania waliokurupuka ambao walikua hawana nia wala habari ya kuoa, waliokusudiwa kwenye tangazo letu hawakusudii hao bali sisi tunaowalenga ni wale walio na wachumba, wameshapeleka posa, pengine wamekubaliwa na wanadawa na wakaondoka kwa kukosa mahali”

Kadhalika Sheikh Kishki alisema muoaji lazima awe tayari kufunga ndoa ya pamoja na ndoa hiyo itafanyika jijini Dar es Salaam.

“Uzuri wa uislamu pale panapofungishwa ndoa si lazima bi harusi awepo kikubwa ni atoe idhini tu ya kukubali kuolewa ila baba mkwe ni lazima awepo na kama asipokuwepo basi atume muwakilishi”

Sheikh Kishki alisema sherti lingine muoaji lazima awe mtanzania, na kijana huyo athibitishwe na imam wa eneo lake kwa barua ili wasiingize watu wasio sahihi kwenye orodha yao.

Sheikh Kishki alisema taasisi hiyo itatoa ofa ya watu 20 kwa upande wa mwanamke na mwanaume, kwa kuwapa kadi 10 ndugu wa kikeni na 10 ndugu wa kiumeni kuja kushuhudia ndoa yao.

Sheikh Kishki Amewataka watanzania kutokubali kuletewa vitu visivyo Vya maana, lakini pia amewataka wanawake na wanaume kuona kuepusha mmomonyoko wa Madili nchini.

“Kwa sasa kuna wimbi la kwenda kinyume na sheria za Mwenyezi Mungu, mwenyezi mungu ametuuma sisi wanadamu tumekuja wawili wawili, lakini mwanamke na mwanamke wanataka waoane na mwanaume na mwanaume wanataka waoane, hata huu mtindo wa kuodhesha vijana ni moja ya kuepusha mmomonyoko wa maadili”.

Mbali na kuwatolea mahari vijana 50, Taasisi hiyo kwa Mwaka jana waliweza kudhamini wanawake wajawazito 100 bila kuangalia imani zao, itikadi zao, makabila yao wala rangi zao ambapo katika hao nusu na robo wamejifungua kwa upasuaji na waliobaki wamejifungua kawaida ambapo taasisi hiyo wamebeba gharama zao.