May 15, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

UNDP yazindua mpango matumizi ya nishati bora nchini

Na Zena Mohamed,TimesmajiraOline,Dodoma

SHIRIKA la Maendeleo la Kimataifa UNDP,limesema limebaini upotevu wa nishati hasa majumbani kwakushindwa kutumia nishati kwa usanifu na kupelekea umeme kutokidhi mahitaji hadi kufikia mgao.

Hayo yamesemwa jijini hapa leo,Machi 15,2024 na Mtaalamu mshauri wa Shirika hilo Robert Washaija ambapo amesema kuwa kutokana na kubaini hayo wameamua kuja na
Mpango wa matumizi ya nishati Bora Tanzania unaoenda Sanjari na Mradi  wa wazo la kibunifu la matumizi sahihi ya Nishati.

Washaija amesema kuwa shindano hilo litagharimu jumla ya  Shilingi Milioni 250 kwa washiriki ambao watachaguliwa  kushiriki kuandaa kazi zao ambazo zitaleta suluhisho la changamoto ya matumuzi yasiyo sahihi ya nishati.

Amesema kuwa mpango huo wa matumizi bora ya nishati unalengo la kuhakikisha nchi iliyopo kwenye uchumi wa viwanda inakuwa na matumizi bora ya nishati.

Ameeleza kuwa mradi huo ni wa kimkakati kuhusu matumizi bora ya Nishati na unafadhiliwa na umoja wa Ulaya na Ubalozi wa Ireland na wanafanya kazi pamoja na Wizara ya Nishati.

“Tunatambua kwamba eneo hili ni geni kwani tukianzia majumbani ni wengi wanapoteza nishati kwa kushindwa kutumia nishati  kwa usanifu na kuweza kutumia nishati kubwa na kuipoteza kwani tungekuwa tunafuata matumizi bora ya nishati tusingekuwa na mgao wa umeme kama tungekuwa na matumizi rasmi ya umeme,”amesema Washaija

Aidha ametaja wadau wengine wanaoshirukiana nao kuwa ni Wizara ya Nishati na wafadhili wao umoja wa Ulaya, Taasisi ya Maendeleo ya Viwanda,Shirika la Viwango Tanzania (TBS),Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS)na Taasisi ya elimu (DIT).

Hata hivyo amesema kuwa moja ya matunda ya mradi huo ni Kujenga uwezo nchini na kuwa na wataalamu wa kisasa ambao wataweza kutoa huduma mbalimbali pale zinapohitajika kuhusu matumizi bora ya Nishati,na kuzijengea uwezo Taasisi mbalimbali pamoja na wafanyakazi wake.

Kwa upande wake Afisa Mahusiano wa UNDP Jolson Masaki amesema kuwa kwenye shindano hilo la kibunifu la matumizi bora ya Nishati nchini wanalenga zaidi vijana wakike na wakiume wenye mawazo ya kibunifu yanayoenda kutoa mchango mkubwa katika kupunguza matumizi ya Nishati

“Ninaposema kupunguza matumizi ya Nishati ina maana kwamba kuna Nishati ambayo tunaitumia vibaya,sasa kupitia mawazo hayo ya kibunifu tutaenda kupokea maoni kutoka kwa Watanzania,”amesema Masaki

Aidha amesema kuwa ili uweze kushiriki katika shindano hili la kibunifu la matumizi bora ya Nishati kitu cha Kwanza lazima uwe na wazo la kibunifu ambalo linahusiana na matumizi bora ya Nishati,Lazima uwe Mtanzania na washindi kumi watachaguliwa ambapo katika hao washindi watapata Milioni Ishirini na tano kwa kila mmoja.

Ameongeza kuwa katika mawazo hayo ya kibunifu wanatazamia kupokea mawazo ambayo yanaweza kupunguza matumizi ya Nishati na mabadiliko ya tabianchi ambayo yamekuwa yakiathiri nchi zetu.

Pia Masaki amesema kuwa wazo hilo la kibunifu la matumizi bora ya Nishati ambalo limezinduliwa leo litakuwa ni la muda wa mwezi mmoja kuanzia leo Siku ya Uzinduzi hadi mwishoni mwa mwezi wa nne.

Kuhusu mwendelezo wa hili shindano la kibunifu la matumizi bora ya Nishati Masaki amesema kuwa huu mradi ni wa muda wa miaka mitatu.

Naye Mhandisi Collins Lwanga Kutoka Wizara ya Nishati amewaomba watanzania wote kuchangamkia fursa hii ya wazo la kibunifu la matumizi bora ya Nishati.

“Tumekuja kushuhudia uzinduzi wa shindano la wazo la kibunifu kuhusu matumizi bora ya nishati nchini ningependa kuwaalika watanzania wote kuweza kushiriki na kuendelea kubuni bunifu zenye tija kwani kila mmoja anatambua umuhimu wa sekta hii ya nishati,”alisema Lwanga.