May 4, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Tulia Trust, Bilal Muslim Mission yatoa huduma ya vipimo vya macho na miwani bure

Na Esther Macha, Timesmajira Online, Mbeya

TAASISI ya Bilal Muslim Mission Tanzania kwa kushirikiana Taasisi ya Tulia Trust wameanza kutoa huduma za huduma za uchunguzi wa awali wa magonjwa ya macho kwa wananchi4, 000, kutoka maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Mbeya.

Huduma hiyo ambayo imeanza kutolewa bure leo ijumaa Desemba 9, mpaka 11,mwaka huu huku Ikisimamiwa na madaktari bingwa 40 ambao matarajio ni kufanya uchunguzi kwa wagonjwa 1,200 mpaka 1,500,kwa siku.

Akizungumza katika eneo la upimaji wa Macho katika viwanja vya Ruanda Nzovwe katika shule ya msingi Kagera , Mratibu wa Taasisi ya Bilal Muslim Mission Tanzania, Ain Sherif amesema kuwa mwitikio wa wana Mbeya ni mkubwa na wanatarajia kufanya upasuaji wa mtoto wa jicho.

Sherif amesema kuwa wanategenea kuwafikia watu 3000 mpaka 4000 na kufanya huduma ya mtoto wa jicho kwa watu 300 kutoa dawa na miwani pamoja na kutoa nasaha.

“Changamoto iliyopo ni kuwa watu hawangalii afya ya macho, ndugu zangu natoa wito watu kufuatilia afya ya macho kwakuwa ni kiungo muhimu kwa binadamu lakini pia watanzania wajenge tabia ya kucheki afya zao” Amesema Mratibu huyo.

Jackline Boaz ni Meneja Tulia Trust mkoa wa Mbeya, amesema kuwa tukio hilo la upimaji linatolewa bure kabisa na taasisi ya Bilal Muslim Mission Tanzania kwa kushirikiana na ofisi ya Mbunge na taasisi ya Tulia Trust.

Amesema kuwa zoezi hilo la upimaji macho litafanyika kwa siku tatu hivyo wananchi wajitokeze kwa wingi kuna madaktari bingwa karibu 40 watakaotoa huduma ya upimaji macho kwa siku zote.

Hawa Mathias ni Mmoja wa waandishi wa habari mkoa wa mbeya waliopima tatizo la macho amesema kuwa watu wengi walikuwa na changamoto ya tatizo la macho lakini walikuwa hawafahamu changamoto hiyo.

“Wananchi wajitokeze kwa wingi kupata huduma ambayo Mh Spika na Mbunge wa Mbeya Mjini amejitolea kuwaleta watalaam wa macho ili kusaidia wananchi wenye changamoto ya macho” amesema Mwandishi huyo.