May 2, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

TNMC yawafutia leseni Wauguzi wawili wa Mtwara

Na Mwandishi wetu, TimesMajira Online, Pwani
 

BARAZA la Uuguzi na Ukunga Tanzania (TNMC) limewakuta na hatia Wauguzi Wanne kati ya Watano wa Hospitali ya Wilaya ya Mtwara Mkomaindo waliofikishwa kwenye kikao cha Baraza hilo, Kibaha Mkoani Pwani ambapo wametoa adhabu kali ya kuwafutia leseni Wauguzi wawili huku wengine wawili wakipewa onyo na kalipio kali.

Akisoma hukumu hiyo Mwenyekiti wa Baraza hilo la Wauguzi na Wakunga Tanzania, Prof. Lilian Mselle mbele ya jopo la Wajumbe wa Baraza hilo sambamba na Wauguzi hao pamoja na ndugu walioshtaki katika shauri lililotokea Mwaka jana, Ambapo Wauguzi  Tumaini Hussein Milanzi na Elizaberth Rashid Njenga wamekutwa na hatia katika kifungu cha 25[3][K] cha sheria ya Uuguzi na Ukunga Tanzania, kwa kushindwa kutimiza wajibu wao wa kumuudumia mgonjwa kwa kiwango kinachotakiwa sawasawa na alichojifunza, hata hivyo wote waliweza kuwasilisha utetezi wao pamoja na maelezo mengine, Mwenyekiti huyo alitoa onyo na kalipio kali kwa kila mmoja wao.

‘’Hukumu yako Tumaini na Elizabeth mmekutwa na adhabu ya kalipio kali, chini ya kifungu cha 28[3] [C], kwa maana hata ukija kufanya kosa dogo kiasi gani utachukuliwa maamuzi tofauti kwa kupata adhabu kubwa zaidi,’’ amesema  Mwenyekiti wa Baraza hilo Prof. Lilin Mselle.

Aidha, Prof. Lilian Masele, amesoma hukumu nyingine kwa Wauguzi Joyce John Mkane na Pascal Arudini Mnyalu, kwa pamoja walikutwa na hatia chini ya kifungu cha sheria cha 25[3][F] na kifungu cha 25[3][K] cha sheria ya Uuguzi na Ukunga Tanzania, kwa kosa la kumtelekeza mama Mjamzito aliyefika Hospitalini kwa lengo la kujifungua,

Pia kushindwa kudumisha viwango vya Kitaaluma, ambapo mgonjwa hakuonwa kabisa kitaaluma.

Hata hivyo katika utetezi wao, Muuguzi Joyce ameomba kusamehewa adhabu kwani alishasimamisha miezi kadhaa baada ya tukio hilo hivyo amejifunza kutokana na kosa, huku kwa upande wa Muuguzi Pascal yeye aliomba asamehewa kutokana na wakati wa tukio hilo alikuwa na changamoto ya Kimahusiano kwenye familia yake hivyo  kupelekea kutofanya kazi kwa ufanisi.

Hata hivyo, Mwenyekiti Prof. Lilian Mselle ametoa hukumu juu ya shauri hilo, alisema 

Licha ya kuwasikiliza pamoja na utetezi wao, wanatoa hukumu hiyo ilikuwa fundisho kwa wengine watakapoona wajue hiyo ndio mifano halisi,

‘’Nyote kwa pamoja, tumewapa adhabu ya kuwaondoa kwenye orodha ya Wauguzi na Wakunga [ROLLS] kwa mujibu wa kifu cha 28[3][A] cha Sheria ya Uuguzi na Ukunga Tanzania namba [1] ya mwaka 2010, kwa maana ya hukumu hii, hamtajishughulisha na shughuli za Uuguzi na Ukunga wakati wote mpaka pale wengine mtakapopata nafasi ya kukata rufaa kulingana na kifungu cha Uuguzi na Ukunga cha [31] ndani ya miezi mitatu,

na rufaa hii inakatwa kwa Waziri mwenye dhamana, hivyo mtapewa kila mmoja nakala ya hukumu,’’ amesema Prof. Lilian Mselle.

Hata hivyo kabla hajahitimisha tukio hilo, aliomba wote waliofikishwa hapo kumuomba msamaha mama mzazi ambaye mwanae aliyepelekwa kujifungua na kupelekea kifo cha mtoto wake,

‘’kwani kifo kinapangwa na Mungu na kinaweza kutokea ila kwa hali hii kingeweza kudhuhirika endapo wangefanya kazi zao kwa kuzingatia miiko.’’ AlmehimishaProf. Lilian Mselle wakati wa kutoa hukumu hiyo, ambapo wakati wote ilitawala vilio na simanzi kwa Muuguzi Joyce hali iliyolazimu wenzake kuungana nae kwa kumshikiria kutoka nae nje  huku akiangua kilio kikali.

Aidha, kwa upande wao ndugu waliopoteza mtoto wao, Wameishukuru Serikali pamoja na Baraza hilo kwa kuweza kutenda haki kwa wao wananchi wa kawaida Mtwara Vijijini huku wakiomba wananchi wengine kuchukua hatua katika tatizo lolote ambalo wataona halijaenda sawa katika masuala ya huduma za afya kutoka kwa Wauuguzi na Wakunga ama wengine.

Tukio hilo, lilitokea tarehe 1 na 2 Novemba 2021, saa tano usiku na siku iliyofuata ilidaiwa Wauguzi hao kushindwa kumuhudumia mgonjwa huyo ambaye alifika kituoni hapo kujifungua akitokea kituo cha Afya cha Kijiji kilichokuwa mbali na Hospitali ambapo alipewa uhamisho wa matibabu zaidi kwenye Hospitali hiyo ya Wilaya.

Hukumu hiyo imesomwa jioni ya tarehe 18 Oktoba 2022,mbele ya Wakili wa Serikali, Hangi Chan’ga , Mwenyekiti wa Baraza la Uuguzi na Ukunga Tanzania, Prof. Lilian Mselle alisema, baraza limewatia hatiani walalamikiwa hao wanne huku mmoja akikutwa hana hatia 

Kwa upande wake Msajili wa Baraza la Wauguzi na Wakunga Nchini, Agness Mtawa amesema kuwa baada ya shauri hilo la Wauguzi wa Mkoa wa Mtwara, pia waliweza kupitia shauri la Wauguzi wa Mkoa wa Arusha.

‘’Tulikuwa na tuhuma mbili, moja mkoa wa Mtwara na moja Mkoa wa Arusha, ambapo Baraza limeweza kutoa maamuzi hayo, ikiwemo kutoa kalipio kali na la kuwafutia leseni wauguzi,

Lakini pia kuna tuhuma tano ambazo bado tunaendelea kuzifanyia kazi. Nawaasa Wauguzi wenzangu kuzingatia sheria ilikuweza kutoa huduma bora.

Mwenyekiti wa Baraza la Wauguzi na Wakunga Tanzania, Prof. Lilian Mselle akitoa maamuzi ya kesi.
Msajili wa Baraza la Wauguzi na Wakunga Tanzania, Bi. Agness Mtawa akizungumzia tukio hilo