October 6, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

TLP kushirikiana na vyama vitakavyomuunga mkono JPM

Na Irene Clemence

MWENYEKITI wa Tanzania Labour Party (TLP), Augustino Mrema, amesema Chama hicho kipo tayari kuungana na chama chochote cha siasa ambacho kitakuwa tayari kumuunga mkono mgombea urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais John Magufuli.

Mrema ameyasema hayo Jijini Dar es Salaam leo wakati akizungumza na waandishi wa habari. Amesema chama hicho kinazo sababu mbalimbali za kuiunga mkono CCM kutokana na kuridhishwa na mwenendo mzima wa utendaji kazi.

Amesema wakati huu wa kuelekea Uchaguzi Mkuu ni vema vyama vikaungana vikiwa na msimamo mmoja. “Wakati huu wa kuelekea uchaguzi mkuu ujao TLP inatoa fursa kwa mwananchi na vyama kujitokeza kugombea nafasi mbalimbali za uongozi ili kumuunga mkono Rais Magufuli na hatmaye aweze kupata ushindi wa kishindo,”amesema Mrema na kuongeza;

“Sisi tupo tayari kuungana na vyama vingine ili mradi tu wakubali kumuunga mkono mgombea wa CCM kwa tiketi ya urais, Magufuli.”

Amesema chama hicho hawana agenda yoyote ya kificho, bali lengo lao kuu ni kuonesha uzalendo na hawana makubaliano yeyote ya kunufaika.

Mrema amesema chama hicho kimeungana kwa kauli moja kuamua kumuunga mkono mgombea CCM bila ahadi yeyote Ile. Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu Itikadi na Uenezi, Emmanuel Allute, amesema baadhi ya sababu zilizowasukuma kumuunga mkono mgombea CCM ni pamoja na kuondoa watumishi hewa, usambazaji umeme vijijini, ukuaji sekta ya elimu na na kuimarika kwa huduma za afya nchini.

“Wapo baadhi ya watu wanazusha eti tumenunuliwa …tunashangaa kwanini tununuliwe sisi Jimbo la Vunjo haliwezi kujifanya kukigawa chama, hatuna agenda yoyote Ile tumeonesha uzalendo na hatufichi lolote katika jambo hili,” amesema Allute.