May 18, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

TFRA / Wadau wa mbolea watoa msaada kwa waathirika wa mafuriko Hanang

Na Mwandishi wetu,Timesmajira Online

MAMLAKA ya Udhibiti wa Mbolea Tanzania (TFRA), imekusanya kiasi cha tani 78.5 za mbolea zenye thamani ya zaidi ya milioni 129 kutoka kwa wadau wa mbolea zitakazokabidhiwa kwa waathirika wa mafuriko ya tope yaliyotokea wilayani Hanang katika mji mdogo wa Katesh mkoani Manyara.

Hayo yamebainishwa na Mkurugenzi Mtendaji wa TFRA Joel Laurent wakati akikabidhi mbolea kwa waathirika wa mafuriko ya tope wilayani Hanang katika mji mdogo wa Katesh.

Ambapo amekabidhiwa kiasi cha tani 65 za mbolea za kupandia na kukuzia zilizotolewa na wazalishaji na wafanyabiasha wa mbolea nchini.

“Nimepokea tani 30 za mbolea kutoka kampuni ua Mbolea ya Taifa (TFC), tani 30 kutoka kampuni ya Uzalishaji wa Mbolea Itracom na kiasi cha tani 5 kutoka kampuni la Mbolea na Uchimbaji madini Minjingu”amesema Laurent

Aidha amesema wanatarajiwa kupokea mbolea za misaada kutoka kampuni ya mbolea ya Staco tani 10, Yara tani 2.5 na tani 1 kutoka kampuni ya mbolea ya Premium.

“Milango iko wazi kwa wadau wa mbolea kufikisha misaada yao itakayowasaidia waathirika wa mafuriko wakati huu wa msimu wa kilimo kutokana na kuwa wakulima walikuwa wamenunua mbolea ambazo hazijazaa matunda kutokana na athari za mafuriko walizokutana nazo,”amesema Laurent.

Akizungumzia hali ya usajili kwenye mfumo wa mbolea za ruzuku, Laurent amesema, wakulima 8449 wa Hanang wamejiandikisha na walishanunua kiasi cha tani 1131.2 za mbolea mpaka wanapopata majanga hayo.