May 3, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

TATURA Ruvuma yaendeleza kasi ujenzi wa barabara

Na Cresensia Kapinga, TimesMajira,Online,Namtumbo

WAKALA wa Barabara Vijijini na Mijini (TARURA) Wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma wameendelea na ujenzi wa barabara kwa kiwango cha changarawe na ujenzi wa madaraja, ambapo katika bajeti ya 2021/2022 zitatumika sh. 754,927,477.28 sawa na asilimia 64 ya bajeti kutoka Bodi ya Mfuko wa Barabara.

Akizungumza na waandishi wa habari jana ofisini kwake Meneja wa TARURA wilayani humo, Mhandisi Fabian Lugalaba amesema mwaka wa fedha 2021/2022 wmetengewa bajeti ya kiasi cha sh. Bilioni 1.1 kwa ajili ya matengenezo ya barabara na utawala.

Amesema kuwa walipokea kiasi cha sh. milioni 500 kutoka mfuko wa Jimbo na sh. milioni 307.9 fedha kutokana na tozo, hivyo wameweza kujenga madaraja pamoja na matengenezo ya barabara kwa kuweka mifereji.

Amesema kuwa bajeti ya 2022/2023 watafungua maeneo ya kilimo na shughuli za kijamii kukamilisha miradi viporo na kuboresha barabara zilizo kwenya hali nzuri ili zisiharibike na kurudisha nyuma barabara hizo hivyo kujikuta zikitumika gharama kubwa kwa ajili ya matengenezo .

Mhandisi Lugalaba ameonesha kukerwa na tabia ya baadhi ya wananchi wanaopenda kufanya shughuli za kilimo kando kando ya barabara na kuziba mifereji inayotoa maji, hivyo kusababisha uharibifu wa barabara.

Amewaomba viongozi wa maeneo husika kutoa elimu kwa wananchi kuhusiana na faida ya kulinda na kutunza miundombinu hiyo.

Kwa upande wao baadhi ya wananchi wameipongeza Serikali kupitia TARURA kwa kazi nzuri ili kuhakikisha miundombinu ya barabara inapitika kipindi chote na hasa maeneo ya vijijini, ambapo hapo awali kabla ya TARURA kuwepo hali ilikuwa mbaya.

Meneja wa TARURA Wilaya ya Namtumbo, Mhandisi Fabian Lugalaba akitoa maelezo ya mradi wa box culvert la Mto Litopanyondo kwenye barabara ya Litola Njaramatata ambayo ni mkombozi kwa wakazi wa vijiji hivyo.
Box Culvert la mto Litopanyondo lililopo kwenye barabara ya Litola Njaramatata wilayani Namtumbo.
Ujenzi wa Daraja la Mto Luegu katika barabara ya minazini Libango wilayani Namtumbo ukiendelea na hadi kukamilika utakuwa limegharimu sh. milioni 700.
Moja ya barabara ya kiwango cha changarawe iliyotengenezwa na TARURA wilayani Namtumbo