April 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

TASAF yajenga bweni la wanafunzi wa kike kuondoa adha umbali mrefu

Na. Mwandishi Wetu, TimesMajira Online, Makete

MAKAMU Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa (USEMI), Dennis Londo ameupongeza Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) kwa kujenga bweni la wanafunzi wa kike katika Shule ya Sekondari Mang’oto wilayani Makete kwa lengo la kuwaondolea changamoto ya kutembea umbali mrefu wanafunzi hao, hivyo kuwawezesha kupata muda wa kutosha wa kuzingatia masomo yao.

Baadhi ya wanafunzi wa Shule ya Sekondari Mang’oto wakiimba wimbo maalum wa kuwakaribisha wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa, wakati wa ziara ya kikazi ya Kamati hiyo iliyolenga kukagua utekelezaji wa Miradi ya TASAF katika Halmashauri ya Wilaya Makete.

Londo amesema kuwa, jitihada za Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) kutekeleza miradi mbalimbali ya kijamii ukiwemo wa ujenzi wa bweni hilo la wanafunzi wa kike katika Shule ya Sekondari Mang’oto, ni kielelezo cha namna Serikali ya Awamu ya Sita inavyozingatia mahitaji ya wananchi wake katika maeneo yenye uhitaji.

Londo ameongeza kuwa, wananchi wanapaswa kumuunga mkono Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan aliyedhihirisha nia yake ya dhati kwa vitendo katika kumkomboa mtoto wa kike kupitia TASAF.

Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa (USEMI), Dennis Londo akizungumza na wajumbe wa Kamati hiyo pamoja na wananchi wa Kijiji cha Ilindiwe mara baada ya kukagua mradi wa ujenzi wa bweni la wanafunzi wa kike katika shule ya Sekondari Mang’oto, wakati wa ziara ya kikazi ya kamati hiyo iliyolenga kukagua utekelezaji wa miradi ya TASAF katika Halmashauri ya Wilaya Makete.

Londo amesema, kamati yake inaunga mkono jitihada hizo za TASAF katika kutekeleza miradi mbalimbali ya kijamii inayowanufaisha wananchi katika sekta muhimu hususani nguvu kubwa ya kuboresha mazingira ya elimu kwa Mtanzania.

Sanjali na hilo, Londo amewashukuru wananchi wa eneo hilo kwa kushiriki kikamilifu katika ujenzi wa bweni la wanafunzi wa kike katika shule ya Sekondari Mang’oto, ambapo nguvu kazi yao imekuwa ni sehemu ya kuunga mkono jitihada za Serikali.

Baadhi ya Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa wakisikiliza taarifa ya Maendeleo ya Mradi wa ujenzi wa bweni la shule ya Sekondari Mang’oto wakati wa ziara ya kikazi ya kamati hiyo iliyolenga kukagua utekelezaji wa miradi ya TASAF katika Halmashauri ya Wilaya ya Makete. Watatu kutoka kulia ni Mkurugenzi Mtendaji wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) Ladislaus Mwamanga.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Makete, William Makufwe amesema, kitendo cha Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) kufadhili ujenzi wa bweni la shule ya wasichana Mang’oto kimesaidia watoto wa kike kupaka elimu bora kwa manufaa yao na yenye tija kwa maendeleo ya taifa.

“Mwenyekiti, bweni hili limejengwa ili kusaidia watoto wa kike, kwani kata hii ya Mang’oto ina milima na mabonde hivyo inakuwa ni ngumu kwa wanafunzi wa kike kutoka katika makazi yao na kufika shuleni kwa wakati, na ndio maana tuliomba TASAF watusaidie kujenga mazingira bora ya kuwapatia elimu wanafunzi wa kike ambao sasa watalala katika bweni hili na kuzingatia vizuri masomo yao,” Makufwe amefafanua.

Naye, Mkurugenzi Mtendaji wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) Ladislaus Mwamanga amesema Kamati ya Kudumu ya Bunge imeridhishwa na utekelezaji mzuri wa miradi ya TASAF inayozingatia viwango vya juu kulingana na thamani ya fedha.

Mwamanga amesema utekelezaji huo mzuri wa miradi ya TASAF unatokana na ushirikiano mzuri walionao Kamati ya USEMI, ambayo imekuwa ikitoa ushauri mzuri uliosaidia TASAF kutekeleza vizuri miradi yake.   Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa (USEMI) imekamilisha ziara yake ya kikazi ya kukagua utekelezaji wa Miradi ya TASAF katika Halmshauri ya Wilaya Mji Njombe pamoja na Halmashauri ya Wilaya ya Makete.

Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa pamoja na wananchi wa Kijiji cha Ilindiwe wakitoka kukagua mradi wa ujenzi wa bweni la wanafunzi wa kike katika shule ya Sekondari Mang’oto, wakati wa ziara ya kikazi ya kamati hiyo iliyolenga kukagua utekelezaji wa miradi ya TASAF katika Halmashauri ya Wilaya Makete.