May 17, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Taka za plastiki kichocheo uchafuzi vyanzo vya maji

Na Esther Macha,Timesmajira,Online, Mbarali

UTUPAJI ovyo wa taka za plastiki kwenye vyombo vya usafiri katika maeneo mbali mbali mkoani Mbeya, imeleezwa kuwa changamoto ya kuchochea uchafuzi wa mazingira katika mitalo na vyanzo vya maji.

Ambapo baada ya matumizi ya plastiki hizo ndani ya vyombo vya usafiri hutupwa kwenye mitalo ya maji na kwenda kuziba kwenye vyanzo vya maji .

Kwani mtu baada ya matumizi hayo hutupa sehemu sizizo sahihi hivyo kuleta uharibu wa mazingira.

Kauli hiyo imetolewa leo na Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbarali,Ofisa Mazingira , Raphael Shitindi wakati akifunga kongamano la siku tano la maadhimisho ya siku ya mazingira duniani liloandaliwa na shirika lisilokuwa la kiserikali linalojishughulisha na uhifadhi wa mazingira(SALIOTA).

Ofisa uhifadhi TANAPA Kanda ya Kusini,Goodchance Chao akizungumza katika kongamano hilo

Ambapo kongamano limefanyika katika viwanja vya shule ya msingi Majenje Kata ya Igurusi wilayani hapa.

Shitindi amesema kuwa imekuwa kawaida watu kwenye vyombo vya usafiri wanapokuwa wametumia makopo hayo hutupa kwenye madirisha wakati magari hayo yakitembea kitu ambacho si sahihi.

Hivyo jamii inatakiwa kuelewa kuwa kuna umuhimu wa kuhifadhi mazingira yao kwa kuhakikisha kuwa wanapinga uchafuzi wa mazingira unaotokana na taka za plastiki hivyo wahakikishe vyombo vyote usafiri vinakuwa na chombo maalum cha kuhifadhia taka ili zisiweze kuleta madhara.

“Taka zinapokuwa kwenye maeneo ya mitalo zinaenda kujaa kwenye vyanzo vya maji na kuziba mitalo ya maji na kuleta athari na kuharibu mazingira , hivyo ni lazima kila mwananchi kuhakikisha anafanya kazi ya kupambana ya uchafunzi wa taka za plastiki katika maeneo yote ya Mkoa wa Mbeya “amesema Kaimu Mkurugenzi huyo .

Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbarali , Raphael Shitindi

Hata hivyo Shitindi amesema kuwa kuna jitihada kubwa zimefanyika katika kupambana na uharibifu wa taka za plastiki na jamii nzima ihakikishe inatumia mifuko mbadala ambayo ni rafiki kwa mazingira ili kuwa na mazingira safi katika maeneo yote huku kwenye vyombo vya usafiri kuwe na chombo maalum cha kuhifadhia taka.

Aidha Mkurugenzi huyo amesema kuwa katika Wilaya ya Mbarali kuna watu wamejitokeza kuhakikisha wanaendeleza taka za plastiki zinazokusanywa kutoka kwenye mazingira yao zinaenda kuchakatwa tena na kuwa malighafi ya kuzalisha bidhaa kama viti na bidhaa zingine muhimu.

Kwani yapo maeneo yanayofanya suala hilo mfano Kata ya Ubaruku ambapo kufanya hivyo ni kulinda mazingira.

Kwa upande wake Ofisa Uhifadhi Tanapa Kanda ya kusini ,Goodchance Chao amesema kuwa wataendelea kutoa ushirikiano ili kuhakikisha mazingira yanakuwa safi na kumtaka Mkurugenzi wa shirika la SALIOTA kutokata tamaa katika mapambano ya uhifadhi wa mazingira .

Aidha Chao amesema taka za plastiki zimekuwa changamoto kubwa lakini kuna juhudi mbalimbali zimekuwa zikifanyika katika kukomesha taka hizo.

Baadhi ya wadau walioshiriki kongamano hilo kutoka maeneo mbalimbali ya wilaya hiyo

Huku akitolea mfano kwa Jiji la Dar-es-Salaam wameweza kukusanya taka hizo na kuzibadilisha kwa kutengeneza vitu vingine katika kuepusha uchafuzi wa mazingira na hata Mkoa wa Mbeya wanaweza kufanya hilo kwani taka hizo za plastiki zina athari kubwa kwenye mazingira yao.

“Kikubwa niwaombe ushirikiano kwani tumekuwa tukipata changamoto kubwa kwenye maeneo ya uhifadhi hasa vyanzo vya maji tumejaribu kutoa elimu lakini bado kwa kiasi fulani ingawa elimu imekuwa endelevu hivyo ndugu yangu Mkurugenzi wa SALIOTA naomba uendelee kutoa elimu mbalimbali kwa wananchi na wadau sababu bado kuna ukataji wa miti ovyo ambayo unasababisha kuongezeka kwa mabadiliko ya tabia nchi,”amesema na kuongeza kuwa

“Bado naona kuna uingizaji wa mifugo kwenye maeneo ya hifadhi ambayo imekuwa ni changamoto kubwa,watu wachache wanaoharibu vyanzo vya maji na walioelimika ni wachache”amesema Ofisa Uhifadhi huyo.

Elisha Mwanikawaga ni Mkurugenzi Mtendaji wa shirika lisilokuwa la kiserikali linalojishughulisha na masuala ya mazingira wilayani Mbarali (SALIOTA)alitoa ombi kwa Halmashauri ya Wilaya ya Mbarali kupatiwa miche ili iweze kuwasaidia kugawa kwa wananchi katika kuhifadhi mazingira katika maeneo mbali mbali wilayani humo .