May 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

T-MARC Tanzania watoa ruzuku kwa kampuni ya Tanz Med

Na Irene Clemence, TimesMajira Online

SHIRIKA lisilokuwa la Kiserikali la T-MARC Tanzania limetoa ruzuku ya shilingi Milioni 50 kwa Kampuni ya Tanz Med inayotoa huduma za afya hapa nchini baada ya kuibuka kidedea katika mradi wa kijana Nahodha

Fedha hizo zitaiwezesha Kampuni ya Tanz Med kwa ajili kuboresha zaidi suluhisho la kibunifu katika kipindi cha miezi sita.

Akizungumza na Waandishi wa habari, Jijini Dar es salaam, wakati wa hitimisho la mafanikio ya tukio la ubunifu (Innovation Lab)kwa vijana wa taasisi tano za Vijana kuwasilisha namna mradi wao unavyofanya kazi Mkuu wa Mradi wa Kijana Nahodha (Youth Captain), Dkt. Tuhuma Tulli

Amesema Taasisi hiyo ilijikita katika kuangalia namna teknolojia inavyoingiliana na afya ya akili na mtu binafsi anavyoweza kukabiliana na changamoto kupitia jukwaa la majadiliano ya pamoja mtandaoni.

“Tunajivunia kuona Washiriki wote ambao wameshiriki wameonyesha nia ya kushiriki katika mradi huu na kwamba vijana wa Tanzania si tu viongozi wa kesho bali pia ni chachu ya mabadiliko chanya ya leo”amesema Dkt Tulli

Dkt Tulli amesema Taasisi hiyo ilioonesha uwezo mkubwa katika kutatua changamoto muhimu zinazowakabili vijana wa Kitanzania.

Mkuu huyo wa mradi aliendelea kueleza kuwa Kupitia mradi wa Kijana Nahodha (Youth Captain) unaendeshwa na Shirika Hilo la T- Marc na kufadhiliwa na
Shirika la Marekani la Maendeleo ya Kimataifa (USAID), umelenga kuwafikia vijana wasio kuwa na ajira.

Amesema jumla ya vijana 45,000 wanatarajia kunufaika kupitia taasisi mbalimbali za Kibunifu za Vijana kutoka Mikoa yote mitano ya Zanziba na Mkoa wa Dar es Salaam na Morogoro.

“Mradi huo umelenga. kuwawezesha vijana wa Kitanzania kwa kupata mafunzo, atamizi (mentorship), na ufadhili wa mradi… kupitia Taasisi za Kibunifu tunazozitaka ambazo zitasaidia vijana na zitazokuwa endelevu na hata taasisi nyingine zinaweza kuchukua ubunifu huo kuuendeleza na kuweza kusaidia Vijana wengi zaidi nchini,”amesema. Dkt Tulli

Aidha amesema lengo la mradi huo ni kusaidia vijana kujiajiri na waweze kuajiriwa pamoja na kuwaunganisha na Makampuni, taasisi mbalimbali kwaajili ya kuwapatia nafasi vijana wabunifu.

Vilevile amesema Mradi huo utawezesha vijana wa Kitanzania kupitia suluhisho bunifu zinazolenga kuboresha ustawi wao wa kijamii, kujumuishwa kiuchumi na afya.

Dkt. Tulli amesema kuwa Vijana 120 walijitokeza ili kushiriki katika mradi huo lakini mchujo ukafanyika kupitia Serikali na T-MARC na kupata kampuni tano ambazo zinamawazo bora ya kibunifu na yanasaidiaa vijana kwa wingi.

Hata hivyo amesema kabla ya tukio hilo mashirika matano yalichaguliwa kati ya zaidi ya mashirika 120 ambayo yaliotuma maombi, na kupatiwa mafunzo/muongozo kwa muda wa miezi sita iliyopita yaliyolenga kuwawezesha kuboresha bunifu zao.

Kwa upande wake Mwakilishi kutoka ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Da es salaam, Dkt Gunini Kamba alilipongeza Shirika la T- mark kwa kuja na mradi wa kijana Nahodha ambao utawasaidia vijana wasio na ajira kujikwamua kiuchumi.

Aidha alitoa wito kwa vijana nchini kuchangamkia fursa ya kujiajiri kupitia bunifu mbalimbali ili waweze kunitegenezea kipato na kujiwezesha kiuchumi.

“Zipo bunifu nyingi ambazo zinaweza kubadilisha maisha ya vijana wengi ambao wamekuwa hawana ajira hivyo hii fursa Kwa kujikwamua”amesema

Naye mmoja wa washiriki watano kutoka Taasisi zilizopata nafasi ya kuwasilisha Bunifu kutoka Taasisi ya Green Composting , Cecil Sagawala amesema Taasisi yake imejikita katika kufanya ubunifu wa kubadilisha taka kuwa mbolea.

Aidha alitoa wito kwa vijana kufanya bunifu mbalimbali ambazo zitaweza kuwa chachu ya mabadiliko chanya katika jamii.

Mkuu wa Mradi wa Kijana Nahodha (Youth Captain), Dkt. Tuhuma Tulli akikabidhi vyeti kwa washiriki wa Mradi wa Kijana Nahodha jijini Dar es Salaam wakati wa hitimisho la mafanikio ya tukio la Ubunifu (Innovation Lab) kwa vijana wa taasisi tano za Vijana kuwasilisha namna mradi wao unavyofanya kazi.
Kiongozi wa Mradi wa Kijana Nahodha (Youth Captain), Dkt. Tuhuma Tulli akizungumza Dar es Salaam wakati vijana wa taasisi tano za Vijana wakiwasilisha namna mradi wao unavyofanya kazi.