May 7, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Serikali yaweka bayana muelekeo wa Kilimo,Mifugo na Uvuvi

Na Penina Malundo, timesmajira

SERIKALI imeweka bayana muelekeo wa Tanzania katika suala la Kilimo ,Mifugo na Uvuvi ambapo sera zake zitasaidia kwa kiasi kikubwa kuzalisha ajira kwa vijana na wanawake.

Pia  imesema kuwa kwa mwaka huu wa fedha imepandisha bei ya chakula kwa zao la mahindi kutoka Sh. 600 hadi Sh. 1000 lengo likiwa ni kumuinua mkulima wa kawaida.

Hayo yalibainishwa jijini Dar es Salaam jana na Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo, Gerald Mweli wa wa mkutano kuelekea Kongamano la Afrika la mifumo ya chakula 2023 linalotarajiwa kufanyika Septemba 5 hadi 8 mwaka huu.

Amesema sababu ya serikali kuwekeza kwa vijana na wanawake katika sekta ya kilimo ni pamoja na kutatua tatizo la ajira katika kuwawezesha kulima,kuwatafuta masoko pamoja na kuwawezesha kupata ardhi.

Amesema msimamo wa Serikali ni kuwawezesha wakulima kumudu gharama za zalishaji na kwamba wataendelea kuhakikisha wanawawekea mazingira mazuri ili waweza kufanya kilimo biashara na kujikwamua kiuchumi.

“Mipango yetu kwa sasa tunawangalia wakulima wadogo, hata sera zetu ni kuhakikisha tunaongeza tija na kuwapatia mazingira mazuri katika kufanya shughuli zao za kilimo.

“Mpaka sasa tumesajili vijana 150 ambao wanajishughuisha na kilimo, mifugo na mazao ya chakula watakaoudhuria mkutano huu hii yote inaonesha ni kwa namna gani Serikali inawajali vijana hawa,” amesema Mweli

Aidha amesema kongamano hilo la Afrika la Mifumo ya Chakula 2023 litakuwa na maeneo matatu ambayo ni maandalizi, mkutano wenyewe pamoja na kuangalia namna ya utekelezaji wa maazimio yatakayotolewa.

Amesema mpaka sasa watu waliojiandikisha kushiriki kongamano hilo wamefikia 3300 ikiwa ni tofauti na mwaka jana wakati wa Kongamano hilo lilofanyika Kigali Rwanda walikuwa washiriki 2000.

“Tumefanikiwa kupata watu wengi hii ni kutokana na namna ambavyo tumejipanga katika kuwashirikisha watu mbalimbali kushiriki wakiwemo wafanyabiashara, wakulima wenyewe pamoja na wawekezaji, “amesema

Kwa upande wake mwakilishi kutoka Benki ya Taifa ya Biashara,  Raymond Urassa amesema benki hiyo ipo tayari kuwasaidia wakulima na kwamba matazamio yao makubwa ni kuwawezesha watu hao kiuchumi na kiteknolojia. 

“Tunaimani kuwa kupitia mkutano huu wakulima watajua namna ya kupata taarifa sahihi za hali ya hewa ili ziweze kuwasaidia kujipanga katika kilimo chao,” amesema.