April 27, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Serikali yatoa milioni 200 kutatua changamoto ya ufinyu wa wodi ya wazazi kituo cha Afya Buzuruga

Na Judith Ferdinand, TimesMajira Online, Mwanza

Katika kuhakikisha huduma za afya ya mama na mtoto Ina kuwa Bora Serikali imetoa kiasi cha milioni 200, kwa ajili ya upanuzi wa wodi ya wazazi katika kituo cha Afya Buzuruga kilichopo Kata ya Buzuruga Wilaya ya Ilemela mkoani Mwanza.

Hiyo ikiwa ni jitihada za serikali katika kuboresha huduma za afya za mama na mtoto pamoja na kutatua changamoto katika kituo hicho cha afya Buzuruga kinachokabiliwa na changamoto ya ufinyu wa wodi ya wazazi ambayo wastani ina uwezo wa kuhudumia wagonjwa 120-180 kwa mwezi lakini sasa wanahudimia wastani wa wagonjwa 500 kwa mwezi pia inakabiliwa na uhaba wa vitanda hali inayowalazimu kulala wagonjwa wawili hadi watatu katika kitanda kimoja.

Akizungumza na timesmajira ofisini kwake Kata ya Buzuruga, Naibu Meya wa Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela,Diwani wa Kata ya Buzuruga Manusura Sadick,ameeleza kuwa changamoto hiyo imekuwa ikisababishwa na ongezeko la watu ambapo wanaenda kupata huduma hiyo kutoka maeneo mbalimbali nje ya kata jirani na nje ya Wilaya ya Ilemela.

Manusura ameeleza kuwa awali kituo hicho kilipangwa kihudumie wananchi wa Buzuruga na Kata jirani, lakini sera ya afya inamruhusu mtu kupata huduma mahali popote pia wote watanzania hauwezi kuwanyima huduma hali hiyo imesababisha ongezeko la watu wanaotaka huduma hiyo kuwa kubwa kutoka sehemu mbalimbali hasa katika jengo la wodi ya mama na mtoto kwa kina mama wanaojifungua.

Ameeleza kuwa tatizo la ufinyu wa wodi ya wazazi limepatiwa mwarobaini ambapo wamepokea fedha kwa ajili ya upanuzi wa jengo la wodi hiyo ambao utachukua takribani mwezi mmoja.

“Kituo hiki wanafanya kazi vizuri ndio maana wagonjwa wengi,changamoto hii ya sehemu ya kujifungulia tumejaribu kushirikiana kuitatua,tayari kilio chetu Rais amekisikia tumepokea fedha kupitia Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela milioni 200,ambazo ni kwa ajili ya kujenga na kupanua wodi ya mama na mtoto,kupitia Mkurugenzi wetu wa Halmashauri tumekubaliana ndani ya mwezi mmoja Juni 16 hadi Julai 30,2022 tunapaswa kuwa tumekabidhi jengo hilo la wodi ya mama na mtoto,ili kupunguza adha hiyo ya ufinyu wa jengo na wagonjwa kulala wawili hadi watatu kwenye kitanda kimoja,”ameeleza Manusura.

Aidha ameeleza kuwa licha ya kupokea kiasi hicho cha fedha hawana maana kuwa changamoto hiyo itakuwa imeisha moja kwa moja,hivyo amewaomba wadau na wananchi kuungana na serikali katika kutatua changamoto iliopo katika kituo cha Afya Buzuruga ikiwemo kuchangia hupagikanaji was vitanda katika wodi hiyo ikiwemo vya kujifungulia, upasuaji na kupumzika kabla na baada ya kujifungua.

Ameeleza kuwa mbali na upanuzi huo Kata ya Buzuruga baada ya kuwa na ongezeko la watu katika kituo hicho na sera ya nchi ni kuwa kila mtaa kuwe na zahanati,wanao mpango kuanzia Julai 1,2022 Mtaa wa Nyambiti katika kata hiyo waanze ujenzi wa zahanati na itakapo kamilika itasaidia kupunguza wagonjwa wengi kwenda kituo cha Afya Buzuruga.

“Kata hii kwa sasa haina zahanati hata moja bali ina kituo cha afya tu,sasa tumeamua kupitia sera ya afya ya kila mtaa kuwa na zahanati tayari tu maeneo ambayo yametengwa kwa ajili ya ujenzi wa zahanati kwaio tunaanza na hiyo ya mtaa wa Nyambiti,baada ya hapo tutakwenda mtaa mwingine,tuna ujenzi ambao unaendelea wa Hospitali ya Wilaya ya Ilemela ambapo itakapo kamilika kwa asilimia 100, na kuanza kutoa huduma itasaidia kituo hicho cha afya Buzuruga pamoja na vituo vingine wilayani humo kipunguziwa mzigo watu wanaoenda kufuata huduma hususani za kujifungua,”ameeleza Manusura.

Kwa upande wake Mganga Mfawidhi wa kituo cha Afya Buzuruga Dkt.William Ntinginya ameeleza,uwezo wa kituo hicho kwa upande wa wodi ya wazazi ni kuhudumia wastani wa wagonjwa 120 mpaka 180 kwa mwezi lakini sasa kinahudumia wastani wa wagonjwa 500. kwa mwezi hali inavyofanya wodi hiyo kuelemewa huku vitanda navyo ni vichache.

Dkt.Ntinginya ameeleza kuwa wodi ya wazazi ina vitanda 8 idara ya mama ambaye ameweza kujifungua,vitanda 7 upande wa wamama wanaosubili kujifungua, vitanda vinne vya sehemu ambayo wa mama wamefanyiwa upasuaji na vitanda vitatu vya kujifungulia.

“Kutokana na ongezeko la kupata idadi zaidi ya wajawazito wanaokuja kujifungua tunapata changamoto ya wazazi kulala zaidi ya mmoja kwenye kitanda kimoja,kwa sasa tuna wastani ya kuhudumia wamama 500 kwa mwezi wa kujifungua,ukiangalia ni kituo cha afya siyo hospitali hivyo kinaelemewa wakati ujenzi wake awali ulikuwa umelenga kuhudumia wamama 120-180 kwa mwezi na tunafanya upasuaji pia ambapo kwa mwezi unaweza kuta tumefanya upasuaji kwa watu 50-60 na ukiangalia vitanda vilivyopo ni vinne tu vya walioweza kufanyiwa upasuaji,”ameeleza.

Ili kuleta tija ya idadi ya wateja wanaoenda kupata huduma hapo ya mama na mtoto imewafanya kufikiria zaidi ili kuweza kupunguza idadi ya wamama wanaolala zaidi ya mmoja kwenye kitanda kimoja kwa kuanza
ujenzi wa upanuzi wa wodi hiyo ambapo tayari serikali na Halmashauri imewasaidia milioni 200 kuweza kupanua jengo la wodi ya uzazi ambapo litasaidia kutoa huduma bora.

Vilevile ameeleza kuwa athari za watu zaidi ya mmoja kulala kitanda kimoja ni hatari kwa afya zao na za watoto kwani kila mtu uwa na maradhi yake na kwa sasa kuna mlipuko wa magonjwa mbalimbali kama corona ambayo inataka watu wakae kwa umbali( social distance),pale unapokuwa na wateja wakati mwingine inakuwa changamoto kuikabili na uwezi kumuamisha mtu kutoka sehemu moja kwenda nyingine kupata huduma hivyo wanawasisitiza wapate chanjo ya uviko-19 itawasaidia kuwakinga pia na ugonjwa huo.

“Madhara ya kulala wawili au watatu ni kuweza kuambikizana magonjwa kama ya uviko-19 na mama mjamzito kushindwa kupumzika vizuri baada ya kujifungua, vitanda kuwa vichache vya kujifungulia wakati mwingine vinatupa changamoto lakini tunaangalia kitanda cha ziada na kinaandaliwa vizuri ingawa uwezi kupata kila mara wamama watano wakasukuma kwa wakati mmoja,”.

Naye baadhi ya wamama walioenda kupata huduma ya mama na mtoto katika kituo hicho cha afya akiwemo Pendo Sospeter,ameeleza kuwa kutokana na uhaba wa vitanda imewalazimu kulala kitanda kimoja zaidi ya mmoja hali inayosababisha kukosa muda wa kupumzika.

” Tunalazimika kulaza watoto kitandani sisi tunakaa chini,wakati mwingine tunapeana zamu ya kulala maana vitanda ni vidogo kulala watatu na watoto wetu haiwezekani,” ameeleza Pendo.

Mmoja wa wajawazito ambaye ameenda kupata huduma katika kituo hicho ameeleza kuwa wanahofia hata kupata magonjwa ya mlipuko hasa uviko-19 kutokana na kubanana kwenye kitanda kimoja watatu.

Hivyo ametoa wito kwa wananchi kuungana na Serikali katika kuhakikisha inaboresha huduma ya afya ya mama na mtoto hasa katika kituo hicho.

Mwaka 2018 Serikali Kuu ilitoa kiasi cha milioni 400 kwa ajili ya kukarabati na uboreshaji wa kituo hicho cha afya Buzuruga Ili kiweze kutoa huduma za dharura,ulilenga kupunguza vifo vya akina mama vitokanavyo na uzazi hasa wakati wa dharura.

Ambapo ulihusisha wodi ya wakinamama,kutunzia maiti, kufulia,maabara pamoja na nyumba ya mtumishi ambapo licha ya jitihada hizo baada ya kuanza kutoa huduma imejitokeza changamoto huyo ya ufinyu wa wodi ya wazazi na Serikali ikaendelea kufanya jitihada kwa kutoa kiasi cha milioni 200 kwa ajili ya upanuzi wa wodi hiyo.

Mganga Mfawidhi wa kituo cha afya Buzuruga Dkt.William Ntinginya, akizungumza na timesmajira ofisini wilayani Ilemela mkoani Mwanza.(Picha na Judith Ferdinand)
Naibu Meya wa Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela,Diwani wa Kata ya Buzuruga Manusura Sadick, akizungumza na timesmajira online juu ya jitihada za serikali katika kuondoa changamoto ya ufinyu wa wodi ya wazazi katika kituo cha afya Buzuruga.(Picha Judith Ferdinand)
Muonekano wa wodi ya wazazi kituo cha afya Buzuruga