April 23, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Serikali yapokea msaada wa vishikwambi 200 kwaajili ya Sensa

Na Penina Malundo,timesmajira, Online

SERIKALI ya Tanzania imepokea msaada wa vishikwambi (tablet) 200 kutoka Umoja wa Mataifa unaoshughulikia Wanawake (UN Women) kwa ajili ya kufanikisha sensa ya watu na makazi inayotarajiwa kufanyika Agosti 23, mwaka huu.

Akizungumza leo wakati wa kupokea msaada huo jana jijini Dar es Salaam Mtakwimu Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Salum Kassim Ali alisema sensa ya mwaka huu itafanyika kwa kidigitali na moja ya vifaa ambavyo zitatumika kukamilisha zoezi hilo ni vishikwambi.

Amesema vishikwambi vinavyohitajika kwa nchi nzima ili kufanikisha zoezi hilo la sensa ni 205,000 tayari wameshaanza kupokea vishikwambi hivyo kutoka kwa wadau mbalimbali wakiwemo wahisani wa maendeleo na kubainisha hivi karibuni wanatarajia kupokea vingine kutoka Serikalini.

Ali amesema kwa sasa wanaendelea na mafunzo kwa wadau mbalimbali ili waweze kupata ujuzi wa kutosha wa kufanikisha zoezi hilo na kuongeza kuwa anawaomba wananchi kuendelea kujiandaa kuhesabiwa

“Niwatoe wasiwasi kuwa maandalizi ya sensa yameshakamilika kwa asilimia 87 kuelekea 90, tumebakiza siku 40 ili tuanze zoezi hili  hivyo wananchi wawe tayari kuhesabiwa kwa ajili ya Serikali kuendelea kuwaletea maendeleo” amesema

Hata hivyo amewashukuru UN Women kwa msaada waliyoutoa kwani sensa ya mwaka huu itafanyika kwa kidigitali na moja ya vifaa ambavyo zitatumika kukamilisha zoezi hilo ni vishikwambi.

Amesema vishikwambi vinavyohitajika kwa nchi nzima ili kufanikisha sensa ni 205,000 lakini tayari wameshaanza kupokea baadhi kutoka kwa wadau mbalimbali wakiwemo wahisani wa maendeleo.

“Vishikwambi hivi 200 waliotoa UN Women vinathamani ya Dola za Marekani 85,000 vinakwenda  kurahisisha zoezi hili la sensa na tunategemea matokeo yatapatikana mapema, lakini hivi karibuni tutapokea vingine kutoka Serikalini, ” amesema 

Aidha amesema hadi sasa maandalizi ya Sensa ya watu na makazi inayotarajiwa kufanyika Agosti 23, mwaka huu yamekamilika kwa asilimia 87.

Naye Kamisaa wa Sensa Zanzibar,  Balozi Haji Hamza amesema vifaa hivyo walivyovipokea vinahitajika katika zoezi hilo la sensa hivyo wanawashukuru wale wote waliofanikisha kupatikana kwa msaada huo.

Naye mwakilishi wa UN Women Tanzania, Oldan Addou amesema wametoa msaada huo kwa lengo la kuisaidia Serikali ya Tanzania kufanikisha zoezi la kuhesabu watu wakiwemo wanawake. 

“Katika kulijali kundi la wanawake tumetoa vishikwambi hivyo 200 vitakavyosaidia kuhesabu watu wakiwemo wanawake ili kuweza kuwaletea maendeleo, ” amesema