May 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Serikali yafanya maboresho Bandari ya Tanga

Na Jackline Martin, TimesMajira Online

Serikali imefanya maboresho ya Bandari ya Tanga kupitia miradi yake miwili ambapo mradi wa awamu ya kwanza wa kuongeza mlango bahari sehemu ya kugeuzia meli na ununuzi wa vifaa uliogharimu kiasi cha Shilingi Bilioni 172.3 umekamilika kwa 100%

Aidha Mradi wa pili ni uboreshaji Gati 2, ambao ulianza Septemba 5, 2020 uliokua wa miezi 22 wenye thamani ya Bilioni 256.8, umekamilika kwa asilimia 99.85 ambapo itakapofika June 1, 2023 asilimia 0.15 iliyobaki itakua imekamilika.

Hayo ameyasema Meneja wa Bandari ya Tanga, Masoud Mrisha wakati wa Ziara ya Waandishi wa Habari iliyofanyika jana katika Bandari ya Tanga Mkoani humo yenye lengo la kujionea shughuli za utendaji kazi wa bandari hiyo.

“Kufikia mwaka 2019 kulianza mradi wa kuboresha Bandari ya Tanga iliboreshwa kwa miradi ya awamu 2, awamu ya kwanza ilianza tarehe 3/8/2019 awamu hiyo ilikuwa ni ya kipindi cha mwaka mmoja na kazi yake ilikuwa ni kuongeza kina cha maji kwenye Mlango Bahari kutoka Km1.7 kuelekea kwenye mlango Bahari ambapo wanaongeza kina cha maji kutoka Mita 3 -13 na upana wa mlango hadi Mita 73, pia kuongeza kina cha maji sehemu ya kugeuzia Meli kutoka Mita3 -13 kwa kipenyo cha mita 800”

“Mradi wa awamu ya 2 ni kuboresha Gati 2 ambayo 1 iliyojengwa mwaka 1914 na 1954 zenye urefu wa mita 450, upande wa mashariki tuliingia majini kwa mita 50 na magharibi mita 92 kuingia kwenye maji na kuongeza kina cha maji kutoka mita3 mpaka 13 ambapo mradi wa awamu ya 2 ulianza septemba 5, 2020 ulikua ni wa miezi 22 wenye thamani ya Bilioni 256.8 ambapo hadi sasa mradi huo umekamilika kwa asilimia 99.85”

Aidha Mrisha amezitaja Faida zinazopatikana baada ya maboresho ya mradi huo ambazo ni pamoja na meli 6 kuingizwa Bandarini hapo lakini pia kuongezenga kwa shehena katika bandari hiyo hali itakayochochea kuongezeka kwa mapato makubwa na kupatikana kwa Kodi.

“Faida zinazopatikana hadi sasa baada ya maboresho hayo ni tumeshaingiza meli 6 zenye urefu wa Mita kati ya Mita 150 -200 kwa kipindi cha miezi mitatu, shehena itaongezeka kutokana na kuhudumia meli kubwa kwani kwa mwaka kabla ya maboresho tulikua na uwezo wa kuhudumia tani 750,000 lakini baada ya maboresho haya tunapoelekea tutakwenda mpaka Tani Milioni 3 kwa mwaka”

“Kabla ya maboresho ya mradi gharama za uendeshaji zilikuwa juu lakini baada ya maboresho gharama za uendeshaji zimeondolewa, kila tani ilikua ni Dola 1.3, pia gharama za mafuta zilizokuwa zinatumika kwenye mashine sasa zimepungua”

Mrisha amesema faida nyingine ni uwezo wa kuohudumia meli kwa siku 4 ambapo awali kulikua na uwezo wa kuihudumia meli ndani ya siku 8.

Mbali na hayo Mrisha amesema bidhaa kubwa wanazosafirisha kwenda nje ya nchi kupitia Bandari ya Tanga ni pamoja na Katani, Kahawa, Mbao na Makademia (Karanga Pori) lakini pia bidhaa kubwa wanazozipokea kutoka nje ya nchi kupitia Bandari ya Tanga ni pamoja na Clinker, mafuta, vipuri mbalimbali vya magari na bidhaa malighafi za viwandani.

Kuhusu mikakati waliojiwekea wao kama Bandari ya Tanga katika kuhakikisha wateja wanakuja kwa wingi, Mrisha amesema wameshirikiana na vyombo mbalimbali vya Habari kuitangaza bandari hiyo na kutoa punguzo ya tozo kwa mteja mwenye mzigo mkubwa ili kushawishi wateja kutumia Bandari hiyo .

Kwa upande wake Afisa Mauzo kutoka Kampuni ya kutoa huduma ya kutoa mizigo Bandarini (TOPMAX LTD), Thurea Khalfan Thurea amempongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kufanya maboresho ya Bandari ya Tanga kwani italeta ongezeko la uchumi nchini.

Amesema baada ya maboresho ya bandari kumekuwepo na ufanisi mkubwa, hivyo aliomba kuwepo kwa muamko wa usafirishaji meli kwa kuleta meli zaidi kwani bado kuna gharama ambayo ipo.

“Tunatarajia kwamba Kama meli kubwa zitaanza kuja basi gharama za usafirishaji zitapungua”

Kuhusu huduma za Banadari Thurea amesema huduma ni nzuri na ni sehemu nzuri ya kufanyia kazi hivyo amewakaribisha waanchi wote waliokaribu na Bandari ya Tanga, kutumia Bandari hiyo ili kuepusha gharama zaidi.

Bandari ya Tanga ilinza kujengwa mwaka 1888 na kukamilika mwaka 1891 kwa kipindi hicho Bandari ya Tanga ilikua inajulikana kwa jina la Marine Jet, Gati la kwanza lilianza kujengwa mwaka 1914 na Gati la 2 lilihengwa mwaka 1954 magati yote haya mawili yalikhwa na urefu wa mita 450.

Pia Bandari ya Tanga inaukubwa wa eneo la Hekta 17 lakini pia tuna maeneo mengine ikiwemo eneo la mwambani Km 6 lenye ukubwa wa Hekta 176 na eneo la Chongoleani ambapo kunajengwa bomba ya mafuta Km28 lenye Hekta 207.

Kadhalika Bandari ya Tanga inabandari ndogondogo ikiwemo Bandari ya Bangani, Kipumbwi, Pwaja na Sahare, tunao wafanyakazi 258 ambapo wanaume 169, wanawake 59.