May 18, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Serikali kuzalisha bidhaa kwa wingi ili kushindana na masoko ya nje

Na Iddy Lugendo, Timesmajira Online

SERIKALI imejipanga kuzalisha na kutengeneza bidhaa kwa wingi za kujitosheleza ili kushindana na masoko ya nje katika kufikia malengo ya viwango vya juu vya maendeleo ya viwanda na biashara hususani kusaidia vijana kupata ajira na kukuza uchumi nchini.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa mbio za polepole katika viwanja vya sabasaba jijini Dar es Salaam Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Abdallah Ulega amesema lengo ni kuhamasisha umma juu ya ununuzi wa bidhaa za viwanda vya Tanzania ili kuleta ushindani wa masoko ya ndani na nje ya nchi na kupanua wigo wa ajira.

‘’Mkakati huu ulioanzishwa na TanTrade wa kuamasisha umma kununua bidhaa za kwetu ni sahihi sana, kwani tunaponunua bidhaa zetu tunasaidia kuleta ushindani wa masoko ya ndani na nje ya nchi na kupanua soko la ndani na kujenga ajira pamoja na kukuza uchumi wa nchi’’. Pia ameongeza kuwa,

‘’Napenda kuwaamasisha wakurugenzi wa halmashauri zetu kuhakikisha tunashirikiana na kuwasapoti wajasiriamali na vikundi vidogo vinavyozalisha viwanda vya maziwa kuwasaidia kurasimisha utaratibu wa maziwa ili watumie vifungashio vya kisasa na sio vilivyopita na wakati.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Maendeleo ya biashara Tanzania (TanTrade) Latifa M. khamisi ameeleza lengo la kuwa na Maonesho ya 7 ya bidhaa za viwanda vya Tanzania, ambayo ni kuwakaribisha na kuwaamasisha watanzania kununua bidhaa zinazozalishwa na viwanda vya Tanzania.

‘’Maonesho haya yana lengo la kuamasisha Wananchi wa Tanzania kuzijua na kuzipenda bidhaa zetu za Tanzania, hivyo naomba nichukue fursa hii kuwaomba watanzania wote walio ndani na nje ya nchi kuwa wazalendo kwa kununua bidhaa za Tanzania na pia kuhudhuria kwa wingi katika maonesho haya na kujionea uzuri na kununua bidhaa hizo’’. Amesema.

Naye Msajili wa Bodi ya Maziwa Tanzania Dkt. George Msalya amesema kuwa biashara ya Maziwa hapa nchini ina thamani ya USD Bil. 1.28, natoa wito kwa wananchi kufikilia biashara za maziwa yanayozalishwa na viwanda vya ndani kwa sababu ni muhimu kununua bidhaa zinazozalishwa na viwanda vya Tanzania ili kujenga uchumi wetu.