May 5, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Serikali kusaidia watoa huduma Bima za mazao

Na Allan Vicent, TimesMajira Online, Tabora

WAZIRI wa Kilimo na Umwagiliaji Hussein Bashe amefurahishwa na juhudi zinazofanywa na mashirika yanayojihusisha na utoaji huduma za bima ya mazao kwa wakulima na kuahidi kuwapa ushirikiano ili kufanikisha malengo yao.wanu kuhakikisha majanga ya asili yanadhibitiwa kikamilifu.

Ametoa kauli hiyo alipokuwa akizindua Muunganiko wa Mashirika ya Bima (Konsotia) jana katika viwanja vya Ipuli Mkoani hapa.

Alisema muunganiko huo ni muhimu kwa kuwa utasaidia kutatua baadhi ya changamoto zilizopo na kuahidi kuwa serikali itaendelea kuwawekea mazingira wezeshi ili kufanikisha malengo yao.

Aidha aliutaka muunganiko huo kupanua wigo wa huduma zake kwa kuhakikisha majanga yote yanayowakumba wakulima yanapata ufumbuzi hasa mabadiliko ya bei wakati wa masoko.

‘Hii ni hatua nzuri ya kuboreshwa kwa huduma za wakulima ikiwemo kutatua changamoto zao hasa wanapopata majanga kama ukame na mvua za mawe, lakini pia muangalie na mabadiliko ya bei katika masoko,’ alisema.

Kwa upande wa Kamishina wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bima (TIRA) Dkt. Baghayo Saqware alieleza kuwa muunganiko huo utasaidia wakulima wengi pindi majanga yatakapotokea. Alisema wamekusanya mtaji wa kutosha kutoka kwenye mashirika mbalimbali ili kuwafikia wakulima nchini kote.

Mtendaji wa Umoja wa Mashirika hayo Elia Kajiba alimhakikishia Waziri kuwa gharama za kulipia bima ya mazao zitaangalia vigezo maalumu kulingana na ukubwa wa mashamba na mapato ya mkulima.

Aliongeza kuwa mamia ya wakulima wamepata elimu ya bima ya mazao kupitia muungano huo ambao umezionduliwa rasmi katika maadhimisho hayo ya Siku ya Ushirika Duniani (SUD) .

Waziri wa Kilimo Hussein Bashe (wa pili kushoto walioketi) akiwa katika picha ya pamoja na Viongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Tabora, Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Christina Mndeme (wa 3 kutoka kulia) na wengine kwenye kilele cha maadhimisho ya Siku ya Ushirika Duniani (SUD) yaliyofanyika Kitaifa Mkoani Tabora kuanzia Juni 26 hadi Julai 1, 2023. Picha na Allan Vicent.