May 14, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Samatta ajiunga rasmi Fenerbahce

INSTANBUI, Uturuki

NAHODHA wa timu ya taifa ya Tanzania, Mbwana Samatta amejiunga na Klabu ya Fenerbahce inayoshiriki Ligi Kuu nchini Uturuki akitokea Aston Villa ya England kwa mkataba wa miaka minne.

Samatta, mwenye umri wa miaka 27 raia wa Tanzania, alijiunga na Aston Villa akitokea Genk ya Ubelgiji mnamo Januari na alifunga mabao mawili akicheza mechi 16 wakati kikosi hicho cha Dean Smith kiliepuka kushuka daraja siku ya mwisho ya msimu.

Hata hivyo, hatma ya Samatta huko Villa Park, msimu huu haikuwa na uhakika na hakucheza kwenye mchezo wowote hadi sasa, akiwa tu benchi lakina hakutumiwa katika ushindi wa 3-1 dhidi ya Burton Albion katika raundi ya pili ya Kombe la EFL wiki iliyopita.

Akizungumza mara baada ya kukamilika kwa dili la kujunga na Fenerbahce, Samatta amesema kupitia kwenye Ukurasa wake wa Instagram kuwa ana furaha kujiunga na klabu hiyo hivyo atahakikisha anapambana ili aweze luwa bora zaidi.

Hata hivyo, ameishukuru klabu ya Aston Villa kwa kumpa nafasi ya kutimiza ndoto zake ya kucheza Ligi Kuu England. amewashukuru mashabiki wa timu hiyo kwa ushirikiano mkubwa waliompa kipindi chote alichokuwa Uingereza.