May 16, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

SAMAF yasherekea siku ya Wanawake kwa kukumbuka Wagonjwa

Na Mwandishi wetu, timesmajira

KATIKA kusherekea siku ya Wanawake Duniani,Taasisi ya Sauti ya Matumaini(SAMAF),imetoa msaada wa mahitaji mbalimbali kwa wagonjwa wa hospitali ya wilaya ya Ubungo.

Akizungumza jana baada ya kukabidhi msaada huo,Mwenyekiti wa Taasisi hiyo,Penina Malundo alisema lengo la kutoa msaada huo kwa wagonjwa wa hospitali hiyo ni kusherekea na kupeana matumaini katika maisha ya kila siku.

Amesema kutokana na wanawake kuwa jeshi kubwa hivyo ni vema kuendeleza utamaduni wa kupendana,kushirikiana na kusaidiana pale mwanamke mmoja anapokuwa chini kusaidiwa kusimama.

Akitaja baadhi ya msaada waliofikisha kwa wanawake hao ni pamoja na Sabuni za Unga,Sabuni za Miche,Taulo za Kike,Pampers za Watoto,Mafuta ya Kupaka,Sabuni za Kuogea,Juice na Biskuti.

”Hii ni awamu ya pili sasa kwa Taasisi yetu kusherekea siku hii ambapo awamu ya kwanza tulikutana na wanafunzi na kuwapatia elimu ya kujitambua hivyo tumeona mwaka huu kuja kusherekea na wanawake wagonjwa wa hospitali ya wilaya ubungo,”amesema.

Kwa Upande wake Mdau wa SAMAF,Madam Irene Kilumanga amesema siku ya wanawake duniani ni siku ambayo wanawake wote wanapaswa kuungana na kusherekea kwa pamoja.

Amesema hakuna kitakachoshindikana endapo wanawake wawili au watatu wakiwekeza nguvu zao kwa pamoja.”Ndio maana leo hii sisi tumewekeza nguvu zetu kwa pamoja na kuamua kuja kusherekea siku hii na wagonjwa wanawake wa hospitali ya wilaya ubungo,”amesema.

Amesema kutoa msaada huo kwa wagonjwa hao ni njia mojawapo ya kuwafariji na kuwatia moyo katika siku hiyo muhimu kwa wanawake.

Naye Mratibu wa Tiba wa Hospitali hiyo ya Wilaya ya Ubungo,Dkt. Julieth Malundo ameishukuru SAMAF kwa kuwatembelea na kuwapatia msaada wagonjwa hao ikiwa ni njia mojawapo ya kusherekea siku ya wanawake duniani.

Ametoa wito kwa vikundi vingine kufika katika hospitali hiyo na kuwatembea wagonjwa.