May 3, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

SAGCOT yatoa elimu sera ya mbegu kwa wadau

Na Mwandishi Wetu, TimesMajira Online, Arusha

KITUO cha Kuendeleza Kilimo Nyanda za juu kusini mwa Tanzania (SAGCOT) imefanya mafunzi ya siku mbili kwa makampuni ya uzalishaji mbegu juu ya sera,sheria na taratibu mbalimbali za mbegu ili waweze kufanya shughuli zao sambamba na maelekeo ya Serikali kwa lengo kuongeza uzalishaji wa mbegu bora hali itakayosaidia kuongeza tija ya mazao kwa wakulima nchini.

Akizungumza na Waandishi wa Habari baada ya kufungua mafunzo hayo yanayofanyika Jijini Arusha, Meneja wa Sera kutoka SAGCOT, Khalid Mgalamo amesema mafunzo hayo yamelenga katika kuwajengea uwelewa kampuni ya mbegu nchini juu ya sera na sheria za nchini na kutoa mapendekezo ya kuboresha sera hizo ili kufanya uzalishaji wa mbegu bora kuboreshwa zaidi.

“Lengo kubwa ni kuwapitisha kwenye sera za mbeguna kujadili changamoto zinazoikabili sekta ya mbegu na kuja na mapendekezo ambayo yanafikishwa katika ngazi husika kwa maamuzi zaidi ili kuboresha mazingira ya uzalishaji mbegu nchini,”alisema Mgalamo

Alisema wazalishaji wa mbegu ni wadau muhimu katika kuendeleza kilimo kwa kuhakikisha mbegu bora zinapatikana kwa wingi kote nchini ili kukidhi mahitaji nakupelekea tija katika uzalishaji mazao yenye ubora kuongezeka na kuingia kwenye soko la ushindani.

“Nchi itakapo jitosheleza kwenye kuzalisha mbegu bora kupitia makampuni ya hapa nchini itawezesha kupunguza uagizaji wa mbegu kutoka nje ya nchi kwa fedha za kigeni,”alisema Mgalamo

Alisema SAGCOT itaendelea kuratibu mafunzo na kikao mbalimbali kwa wadau wake na taasisi za Serijali kwa lengo la kujadili changamoto na kuja na mapendekezo yatakayo saidia kuboresha sekta ya kilimo,mifugo na uvuvi hapa nchini.

“Mbegu ndiyo kiungo katika kilimo bila mbegu hakuna kilimo hivyo kuna kila sababu ya kushirikiana pamoja kama wadau wa sekta hii kuhakikisha mazingira ya uzalishaji kwa makampuni ya ndani yameboreshwa ili wazalishe mbegu kwa tija,” alisema

Bw.Mgalamo aliongeza kuwa kampuni za mbegu ni sehemu ya kuzalisha ajira kwa vijana hapa nchini sambamba na kuongeza tija ya uzalishaji katika sekta ya kilimo.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji Tanzania Seeds Traders Association (TASTA), Baldwin Shuma alisema mafunzo hayo ni muhimu kwani yanazidi kuboresha sekta zaidi tunaiomba Serikali kuhakikisha wanatenga maeneo katika halmashauri ili makampuni ya mbegu yaweze kupata ardhi ili wafanye uzalishaji wao ambao utakuwa na tija kwa kuhakikisha mbegu bora zinapatikana kwa wingi hapa nchini na kupunguza uagizaji wa mbegu kutoka nje ya nchi.

“Tunaiomba Serikali katika halmashauri zetu kutenga maeneo kwa ajili ya kampuni ya mbegu kufanya uzalishaji wa mbegu kuwa na uhakika wa ardhi ya kufanyia uzalishaji wa mbegu jambo litakalomjengea mwekezaji uhakika wa biashara yake,”alisema Bw.Shuma

Naye Mkuu wa Kitengo cha Majaribio ya Kitaifa ya Umahiri wa Mbegu kutoka TOSCI, Dkt. Adolf Saria amesema SAGCOT inafanya kazi nzuri katika kuunganisha wadau katika kujadili changamoto mbalimbali katika sekta ya kilimo kupitia vikao kama hivi ambapo mapendekezo yatakayopatikana yatakwenda kusaidia katika kuboresha sekta.

“TOSCI ipo katika kutoa ithibati ya mbegu hivyo itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali wa kilimo kuhakikisha mbegu zinazozalishwa zinakidhi viwango vya ubora ili kuongeza uzalishaji wa mazao,”alisema Dkt.Saria

Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Bytrade (T) ltd, Harish Dhutia ameishukuru SAGCOT kwa kumwalika katika mafunzo hayo na kusema mafunzo kama hayo yanaonyesha dhamira ya kweli katika kuboresha sekta ya kilimo nchini.

Mafunzo haya ya siku mbili yamefadhiliwa na Taasisi ya Alliance for a Green Revolution in Africa (AGRA) yambayo yamekutanisha taasisi mbalimbali za Serikali TOSCI, TASTA, TRA, Wizara ya Kilimo, ASA, TARI, TAEC na makampuni mbalimbali ya mbegu nchini.

Mkurugenzi Mtendaji wa Tanzania Seeds Traders Association (TASTA) Baldwin Shuma akizungumza katika mafunzo ya siku mbili ya sera ya mbegu kwa makampuni ya mbegu nchini yaliyofanyika jijini Arusha jana .Mafunzo hayo yameandaliwa na Kituo cha Kuendeleza Kilimo nyanda za juu kusini mwa Tanzania(SAGCOT) na Kufadhiliwa na Taasisi ya Alliance for a Green Revolution Africa(AGRA).

Wajumbe kutoka makampuni mbalimbali ya mbegu nchini pamoja na taasisi za Serikali wakifuatilia mada kwenye mafunzo ya siku mbili ya sera,sheria na kanuni za mbegu yaliyoandaliwa na Kituo cha Kuendeleza Kilimo Nyanda za Juu kusini mwa Tanzania(SAGCOT). Mafinzo hayo yamefanyika jijini Arusha jana na yamefadhiliwa na Taasisi ya Alliance for a Green Revolution Africa(AGRA).
Mkurugenzi Mtendaji wa Tanzania Seeds Traders Association (TASTA) Baldwin Shuma (kulia) akijadiliana na Meneja wa Sera wa Kituo cha Kuendeleza Kilimo nyanda za juu kusini mwa Tanzania( SAGCOT) Khalid Mgalamo(katikati) mara baada ya kufungua Mafunzo ya siku mbili ya sera ya mbegu kwa makampuni ya mbegu nchini yaliyofanyika jijini Arusha jana . Mafunzo hayo yamefadhiliwa na Taasisi ya Alliance for a Green Revolution Africa(AGRA).