May 10, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

RITA yatoa vyeti vya kuzaliwa zaidi ya 300 nanenane

Na Agnes Alcardo, Timesmajira Online, Mbeya.

ZAIDI ya watu 300, wamepatiwa vyeti vya kuzaliwa, kupitia Maonesho ya Kimataifa ya Wakulima, maarufu NaneNane, yaliyohitimishwa jana na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt Samia Suluhu Hassan katika Viwanja vya John Mwakangale Mkoani Mbeya.

Vyeti hivyo vilitolewa na Kabidhi Wasii Mkuu na Mtendaji Mkuu wa RITA, Frank Kanyusi na Naibu Kabidhi Wasii Mkuu ,Irene Lesulie ambapo pia walitoa elimu kuhusu kusajili vyeti vya kuzaliwa wosia kwa wananchi hao.

Baadhi ya wananchi waliokabidhiwa vyeti hivyo,Anitha Mwakilasa amesema kuwa imekuwa fursa nzuri kupita katika banda hilo kwani amepata cheti cha kuzaliwa lakini pia amepata elimu kuhusu masuala ya wosia na ndoa.

“Nilipopata nafasi nikasema tu ngoja nijaribu kufuatilia, ingawa sikuwa na uhakika lakini nashukuru Mungu nimefanikiwa kupata cheti changu hiki hapa lakini kumbe ukija hapa unaweza kupata na elimu pia,”amesema Mwakilasa.

Kwa upande wake Stani Ngimba ambaye naye amepata cheti cha kuzaliwa katika maonesho hayo amesema kuwa alipokwenda kwenye banda la rita amepata elimu ya wosia ambayo a imemuondoa hofu kuhusu kuandika wosia .

“Siku zote nilikuwa nasema nitaandika wosia kesho, lakini kutokana na elimu niliyoipata hapa RITA leo hii naenda kuandika wosia kwani wosia siyo uchuro,”amesema.