April 27, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

ATE, ILO wajadili masuala ya UKIMWI mahala pa kazi

Na Mwandishi, TimesMajira Online

Chama Cha waajiri Tanzania (ATE) kwa kushirikiana na shirika la kazi Duniani (ILO) wamefanya mkutano wa majadiliano wa Sekta Binafsi na wadau na kujadili mchango wa Sekta Binafsi katika kuzuia maambukizi ya UKIMWI katika maeneo ya kazi kupitia uhamasishaji wa umuhimu wa afya na usalama katika maeneo ya kazi Hii ni katika kutekeleza mpango mkakati wa Dunia wa kumaliza Janga la UKIMWI ifikapo mwaka 2030.

Akizungumza na waandishi wa Habari leo Jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mkuu wa Chama Cha Waajiri Tanzania, Suzanne Ndomba amesema mkutano huo unaenda sambamba na mafunzo ya siku tatu ya wakufunzi wa rika yatakayoenda sambamba na kaulimbiu isemayo ‘Mafunzo kwa waelimishaji rika katika mapambano dhidi ya UKIMWI’

Ndomba amesema pamoja na hatua kubwa ambazo Tanzania imepiga katika kutokomeza UKIMWI, bado kuna kazi kubwa ya kufanya na wadau wote ili kupata Tanzania isiyo na VVU/UKIMWI.

“Suala la kutoa elimu kuhusu kupambana na magonjwa ambukizi na yasiyoambukiza bado linahitajika ili kuepukana na uwepo wa magonjwa hayo mahala pa kazi lakini pia wafanyakazi wajitokeze kupata elimu hiyo”

Ndomba amesema wao kama ATE wanaendelea kutoa mchango mkubwa katika kuzikutanisha Sekta Binafsi na wadau kupitia programu mbalimbali za afya na masuala ya UKIMWI katika maeneo ya kazi.

“Chama Cha waajiri Tanzania kama mdau husika katika Sekta Binafsi kwenye masuala mazima ya kutoa uelewa na masuala mzima yanayohusu UKIMWI kwa upande wa Sekta Binafsi hivyo kwa kushirikiana na wadau tunafanya mkutano huu ili kuhakikisha tunaendelea na dhima ya kuendeleza kutoa uelewa na uzoefu katika masuala ya UKIMWI hasa mahala pa kazi”

Kwa upande wake Afisa Program Mwandamizi kutoka Shirika la Kazi Duniani Kanda ya Afrika Mashariki (ILO),Edmund Moshi amesema katika utekelezaji wa afya mbalimbali za eneo la afya bado kuna mambo mengi ya kufanya ikiwemo kuendeleza juhudi za kuhakikisha kwamba UKIMWI unaisha lakini pia pale ambapo upo watu wanaendelea kupewa msaada wanaohitaji ili kuendelea kuwa na Tija mahali pa kazi.

Aidha amesema ILO wanawajibika kikamilifu kuhakikisha kwamba nchi wanachama wanawasaidia kufikia malengo na kuwajengea uwezo kuhakikisha kwamba wanafikia malengo ya nchi na Kimataifa.

Naye Katibu Mkuu wa shirikisho la vyama vya wafanyakazi nchini (TUCTA), Herry Mkunda amewaomba wadau wote kuendeleza ushirikiano katika Kuhamasisha masuala ya UKIMWI, afya na Usalama mahala pa kazi ili kufikia malengo ya mkakati wa 95% hadi kufikia mwaka 2030.

“Katika sehemu ya kazi tunatakiwa tulinde sana wafanyakazi kwasababu muajiri hawezi kupata faida kama wafanyakazi hawana afya nzuri kwahiyo pamoja na mambo mengine isiwe UKIMWI pekee bali hata magonjwa mengine yasiyoambukiza, hii itaweza kuondoa changamoto ya Afya sehemu ya kazi”

“Tunaomba waajiri wahakikishe kwamba ili kuwe na juhudi endelevu wahakikishe wanaweka Mipango ya kupambana na UKIMWI sehemu za kazi kama sehemu za bajeti zao lakini pia kuwe na utaratibu maalumu wa kupambana na magonjwa yasiyo ya kuambukizaMkunda Aliongeza kwa kuwaomba Chama Cha waajiri Tanzania (ATE), kuendelea kutoa elimu Si tu kwa magonjwa ambukizi bali pia magonjwa yasiyoambukiza sehemu za kazi.

Mkutano huo ulihudhuliwa na wadau mbalimbali wa masuala ya UKIMWI kutoka ndani na nje ya nchi ambapo ulienda sambana na kaulimbiu isemayo ‘UKIMWI bado ni Ajenda Endelevu