April 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mkuu wa Mbeya Albert Chalamila

Rc Mbeya abadili mawazo kuhusu ubunge baada ya kauli ya Rais Magufuli

Na Esther Macha, Timesmajira,Online, Mbeya

MKUU wa Mbeya, Albert Chalamila amesitisha azma yake ya kwenda kugombea Ubunge wa Jimbo la Iringa na badala yake ameamua kubaki  mkoani Mbeya kuwatumikia  wananchi kama ambavyo Rais Dkt John Magufuli alimuamini na kumpa ridhaa.

Chalamila ametoa kauli hiyo alipokuwa akizungumza na Waandishi wa Habari wa Mkoa wa Mbeya ambapo amesema Rais Magufuli alimuamini na kumpa ridhaa hivyo nia yake ya kwenda Iringa mjini kugombea ubunge ameihairisha kuanzia sasa.

Amesema kuwa ni kweli awali alikuwa na nia ya kugombea Ubunge Iringa Mjini na kusema kuwa siku zote binadamu ameumbuiwa matamanio na matarajio na msingi wake ni kuyasimamia.

“Ukweli ni kwamba nilijiandaa kugonbea Ubunge Jimbo la Iringa mjini lakini kutokana na maneno aliyoyatoa Rais Magufuli yamenifikirisha sana kuona sina sababu ya kumuangusha yule aliyeniamini na kunipa ridhaa ya kuwatumikia wanambeya kanzia leo nimesitisha uamuzi huo,” amesema Chalamila.

Ameongeza kuwa katika kipindi kifupi kilichopita, Rais Magufuli alitoa fedha nyingi kwa ajili ya kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo ambayo inahitaji usimamizi wa karibu ili zifanye kazi iliyokusudiwa.

Aidha Chalamila amesema kwamba lengo lake lilikuwepo Chama Cha Mapinduzi kupitia Mwenyekiti wake Rais Magufuli ameeleza msimamo wake kuwa ukiomba ruhusa leo kesho anateua mtu mwingine sasa pamoja na kuteua mtu mwingine itakuwa ni utovu wa nidhamu kwa Mkuu wa Mkoa wa Mbeya kutosikiliza ya Mkuu na badae kuja kuvunjika guu.

Hata hivyo Chalamila amesema Mbeya kuna mambo mengi yamefanyika na ambayo yanahitaji usimamizi mfano suala la mapato ambapo wakati anafika Mbeya nilikuta bil.7 zimekusanywa  na kwamba mpaka sasa tumeenda vizuri hivyo hicho ni kigezo tosha ambacho natakiwa kuendelea kusimamia miradi ya maendeleo ya wananchi.

Amesema endapo ataondoka kwenda kugombea ubunge hatakuwa amemtendea haki Rais Magufuli kwani miradi hiyo inapaswa kusimamiwa  na miradi isipokamilika mimi nikiwa sipo  itakuwa ni utovu wa nidhamu na nitapaswa kufungwa kwa uzembe.

Baada ya maelezo hayo, Chalamila ameahidi kuendelea kuchapa kazi huku akiunga mkono jitihada zinazofanywa na Chama cha Mapinduzi (CCM) kwa kuhakikisha Jimbo la Mbeya mjini linarudi mikononi mwa chama tawala.

“Nitaendelea kuchapa kazi lakini niwaambie wale wapinzani kuwa Wanambeya sasa wameamka hawanunui tena kifurushi la tigo kwenda voda badala yake ni tigo kwenda tigo,” amesema Chalamila.