May 18, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

RC Makalla apokea mpango kazi wa zoezi la anuani za makazi DSM

Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Amos Makalla amewaelekeza Wakurugenzi wa Halmashauri zote za Mkoa huo kuharakisha Mpango kazi wa operesheni ya zoezi la anuani za Makazi ambalo ndio Msingi mzuri wa kufanikisha Zoezi la Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2022 inayotaraji kuanza mwezi wa nane mwaka huu.

RC Makalla ametoa maelekezo hayo wakati wa Kikao kazi Cha kupokea taarifa na Mpango kazi wa zoezi la anuani za Makazi ambapo amesema Mpaka kufikia April 14 zoezi hilo liwe limekamilika ili kuenda sambamba na maelekezo ya Rais Samia alietaka Hadi kufikia mwezi wa tano kila kitu kiwe tayari.

Aidha RC Makalla amesema zoezi hilo lina manufaa makubwa kwakuwa linakwenda kuweka Jiji katika mpangilio mzuri, kupunguza Migogoro ya Ardhi, suala la ulinzi na usalama, majanga ya Moto na kuwezesha biashara kidijitali hivyo ametoa wito kwa Wananchi kulipokea vizuri.

Hata hivyo RC Makalla amempongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuleta zoezi hilo kwa wakati muafaka ambao Kuna Mapinduzi makubwa ya sayansi na teknolojia na Mambo mengi yanakwenda kwa mfumo wa digital.

Zoezi la anuani za Makazi kwa Mkoa wa Dar es salaam litahusisha Wilaya zote tano ambapo Wilaya ya Ilala Jumla ya Kata 36 na Mitaa 159, Temeke kata 23 na mitaa 142, Kinondoni kata 20 na Mitaa 106, Ubungo kata 14 na Mitaa 90 na Kigamboni Kata 9 na Mitaa 67.