April 30, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

RC Chalamila: Sitaki kuona mkandarasi msanii ndani ya DSM

Na Heri Shaaban, TimesMajira Online

MKUU wa Mkoa Dar es Salaam Albert John Chalamila ,amesema ndani ya mkoa huo, hataki kuona wakandarasi wasanii, wanaosumbua wakipewa kazi ya Ujenzi wa Miradi, huku akibainisha kuwa umefika wakati kwa Wakandarasi Wazawa kuanza kupewa kipaumbele cha Utekelezaji wa miradi mbalimbali hususani ile iliyoko kwenye Sekta ya Ujenzi.

Mkuu huyo wa mkoa Albert Chalamila, amesema hayo wakati akiweka jiwe la Msingi katika ujenzi wa shule ya Sekondari Mangaya iliyopo manispaa ya Temeke itakayokua na Ghorofa tatu ambayo inajengwa kwa zaidi ya Shilingi milioni 800 ikiwa ni siku ya kwanza ya ziara yake ndani ya mkoa wa Dar es Salaam, ziara inayolenga kukagua utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kuzungumza na Wananchi.

“Katika mkoa wangu sitaki usanii kazi yetu kubwa ni kusimamia miradi vizuri na uwiano wa vifaa vya ujenzi ambapo, kwa hiyo naomba wakandarasi wanaofanya vizuri katika mkoa huu hususani wazawa wapewe kipaumbele sitaki usanii, ujenzi huu wa sekondari mpya ya Mangaya iliyopo Mbagala Mkandarasi amefanya vizuri nampongeza Mkuu wa wilaya na Mhandisi” alisema Chalamila.

Mkuu wa Mkoa Chalamila amewataka Wilaya Temeke kujipanga vizuri kwa ajili ya maendeleo ya wilaya ya Temeke yanayofanywa na Serikali, huku akishauri wananchi waungane na Mbunge wao Abdalah Chaurembo ili kujiletea maendeleo.

Aidha amesema katika mkoa huo, maeneo yamejaa hivyo wakipata pesa wajenge shule za Ghorofa, ambapo anaweza kuja kuzindua Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan au Waziri Mkuu Kassim Majaliwa.

Katika hatua nyingine Chalamila ameagiza Jeshi la Polisi kufuatilia wezi wa Vifaa vya ujenzi katika hospitali ya Ghorofa sita Mbagala Zakhiem ambapo inadaiwa kuna vifaa vinaibiwa.

Wakati huo huo Chalamila ameagiza Watumishi katika Sekta ya Afya kufanya kazi kwa Weledi ili kuondoa malalamiko ya Wagonjwa, Serikali kwa sasa inatafuta eneo ambalo kutajengwa hospitali ya Wilaya ya Temeke, ambapo tayari limebwa eneo la Hospitali ya Taifa Muhimbili lililopo Chamazi Wilayani Temeke.

Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Mbagala Abdalah Chaurembo ametoa malalamiko kuhusiana na Hospitali ya Mbagala ZAKHIM idara ya huduma kwa wateja kulalamikiwa, huku akimuomba mganga mkuu kutatua kero hiyo malalamiko yamekuwa makubwa kwa wagonjwa.

Katika ziara ya mkoa wa mkoa Albert Chalamila wilaya ya Temeke leo ametembelea miradi ya shule ya sekondari, Hospitali ya Mbagala ZAKHIM, mradi wa kupoza Umeme ,Barabara ya Chamazi na mkutato wa kuongea na wananchi Chamazi.