
Puma Tanzania yazindua kituo cha 100
Na Mwandishi Wetu, Timesmajira Online. Tabora
KAMPUNI ya Nishati ya Puma Tanzania imezindua rasmi kituo chake cha 100 cha huduma za mafuta, ikiwa ni hatua muhimu katika upanuzi wa mtandao wake nchini na kuendelea kuthibitisha dhamira yake ya muda mrefu ya kuchangia maendeleo ya kiuchumi na kijamii nchini Tanzania.
Kituo hicho kipya na cha kwanza mkoani Tabora, kimezinduliwa rasmi na Mkuu wa Wilaya ya Tabora, Upendo Wella, aliyeambatana na viongozi wengine wa Serikali, wawakilishi wa wananchi, wateja pamoja na viongozi na menejimenti ya kampuni ya nishati ya Puma Tanzania.
Uzinduzi huu unadhihirisha dhamira yake ya uwekezaji endelevu wa kampuni katika kuimarisha upatikanaji na uhakika wa nishati salama kote nchini Tanzania. Kikiwa kimejengwa katika eneo la kimkakati mjini Tabora, kitovu kinachokua cha kilimo, biashara na usafirishaji, Kituo hiki kipya kitahudumia wafanyabiashara wa ndani na wa sekta ya usafirishaji, huku kikizalisha fursa za ajira mkoani humo.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya nishati ya Puma Tanzania, Fatma Abdalla, alisema hatua ya kufikisha vituo 100 inaonesha imani ya Kampuni katika mustakabali wa Tanzania na dhamira yake ya kujenga thamani ya kudumu kwa jamii inazozihudumia.
“Kufikisha kituo chetu cha 100 cha huduma za mafuta ni zaidi ya kupanua mtandao wetu. Ni ishara ya kukua kwa ushirikiano wetu wa muda mrefu na Tanzania, imani ambayo wateja wetu wameendelea kutupatia na imani yetu ni kwamba, upatikanaji wa mafuta ya uhakika unawezesha fursa na maendeleo,” alisema Abdalla.
“Kila uwekezaji tunaoufanya unaimarisha miundombinu inayowezesha biashara, kuunganisha jamii na kuchangia ukuaji wa uchumi wa nchi. Tunapoelekea mbele, tutaendelea kuwekeza katika kutoa suluhisho salama, bora na za uhakika za nishati huku tukijenga thamani ya kudumu kwa wananchi na jamii tunazozihudumia,” aliongeza Abdalla.
Ikiwa ni sehemu ya uzinduzi wa kituo hicho, Kampuni ya nishati ya Puma Tanzania ilitekeleza shughuli mbalimbali za kijamii zilizolenga kusaidia elimu, vijana na uhifadhi wa mazingira. Shughuli hizo ni pamoja na kutoa mahitaji ya jamii ya Tabora na kuhakikisha kuwa uwekezaji wa Kampuni unaacha athari chanya zaidi ya huduma za kituo cha mafuta.

Aidha Puma Energy Tanzania ilitoa magodoro 100 katika Kituo cha Kulelea Watoto cha Istiqaama kwa lengo la kuboresha mazingira ya maisha ya watoto wanaoishi katika kituo hicho.
Pia Kampuni ilitoa madawati 100 katika Shule ya Msingi Usule, iliyopo Kata ya Mbugani, Halmashauri ya Manispaa ya Tabora. Msaada huo utasaidia kupunguza changamoto ya upungufu wa madawati na kuwawezesha wanafunzi kupata mazingira bora na salama zaidi ya kujifunzia. Pia kwa kushirikiana na shule hiyo pamoja na wananchi wa eneo hilo ilipanda miti 100 katika mpango unaolenga kuchangia juhudi za uhifadhi wa mazingira na kuunga mkono mustakabali wa Tabora yenye mazingira bora na endelevu.
“Katika kampuni ya nishati ya Puma Tanzania, tunaamini mafanikio ya biashara na maendeleo ya jamii yanaenda sambamba. Mipango tuliyoitekeleza hapa Tabora inaonesha dhamira yetu ya kuwekeza katika jamii tunazozihudumia na kushughulikia mahitaji yanayogusa maisha ya wananchi. Kwa kuboresha mazingira ya kujifunzia, kusaidia watoto wanaohitaji msaada na kuhamasisha utunzaji wa mazingira, tunalenga kutoa mchango wa vitendo na wa kudumu sambamba na uwekezaji wetu katika miundombinu ya nishati,” alisema Abdalla.
Akizungumza katika hafla hiyo, mkuu wa wilaya hiyo, Wella, aliipongeza Kampuni ya Nishati ya PUMA kwa kufikia hatua hiyo muhimu na kuukaribisha uwekezaji wa Kampuni katika mkoa huo.
“Uzinduzi wa kituo cha 100 cha kampuni ya nishati ya Puma Tanzania ni hatua muhimu inayoonesha imani ambayo wawekezaji wanaendelea kuwa nayo katika uchumi wa Tanzania,” alisema Wella.
“Uwekezaji kama huu unaimarisha miundombinu yetu, unaleta fursa za ajira, unaunga mkono biashara za ndani na kuchangia maendeleo endelevu ya jamii zetu. Tunaikaribisha Kampuni ya nishati ya Puma Tanzania kuendelea kuwekeza mkoani Tabora na tunahamasisha kampuni nyingine kutumia fursa zilizopo katika mkoa wetu.” aliongeza.

More Stories
Taasisi za umma zatakiwa kuachana na utendaji wa mazoea ili kufanikisha Dira 2050
Maboresho sheria yaongeza ushiriki wa watanzania kwenye migodi
Wizara ya Afya yatoa elimu elekezi huduma za afya