May 4, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

PSSSF yatoa miche ya miti kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi

 

 NA K-VIS BLOG/KHALFAN SAID, DAR ES SALAAM

Katika kutambua na kuunga mkono juhudi za Serikali katika kukabiliana na mabadiliko ya Tabianchi, Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) umetoa miche kwa wastaafu watarajiwa wa Mfuko huo waliokuwa wakihudhuria semina elekezi ya kujiandaa na maisha ya kusataafu utumishi wa Umma.

Semina hiyo ambayo ilifunguliwa Septemba 11, 2023 na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu), Mhe. Profesa Joyce Ndalichako, imefungwa Septemba 12, 2023 na Mkurugenzi Mkuu wa PSSSF, CPA. Hosea Kashimba.

CPA. Kashimba alisema, PSSSF inatarajia kuwa na wastaafu 11,000 katika mwaka wa fedha wa 2023/24 na zoezi la ugawaji miche pia linafanyika kwenye mikoa mingine ambako nako wastaafu watarajiwa wa Mfuko huo wanapatiwa semina kama hiyo.

“Mfuko umepanga pia kugawa miche hiyo kwa wanachama wake 739,000 kote nchini.” Alisema

Akihutubia katika kongamano la Mabadiliko ya Tabia Nchi lililofanyika jijini Nairobi Nchini Kenya, Septemba 6, 2023, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, alisema kuna hatari kubwa, na hatua inapaswa kuchukuliwa sio kesho bali leo na haswa sasa ili kukabiliana na mabadiliko ya Tabianchi.

Tayari Jumuiya ya Kimataifa imemtambua Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambapo Septemba 12, 2023 Bodi ya Ushauri ya Kituo cha Dunia cha Uhimilivu wa Mabadiliko ya Tabianchi (Advisory Board of the Global Centre on Adaptation – GCA), imemteua kuwa Mjumbe wa bodi hiyo.

Akieleza zaidi kuhusu umuhimu wa kupanda miti, Mkurugenzi Mkuu huyo wa PSSSF alisema  “Upandaji miti unasaidia sana katika kukabiliana na janga hili la mabadiliko ya Tabianchi ambayo ni hatari si kwa mazingira peke yake bali hata viumbe vilivyopo katika mazingira haya, tukiwemo na sisi binadamu.” Alisema CPA. Kashimba

“Pia kwa kushirikiana na watumishi wa Mfuko tutaendesha kampeni ya kuhakikisha kila mtumishi anapanda na kuitunza miche kumi ya miti, kampeni hii itaendelea hadi Disemba 2023 ambako tunatarajia tutakuwa tumepanda miche takribani million 7.

“Hivyo ili kuanza kampeni hii mahsusi, katika semina hii kila mwanasemina na wafanyakazi watapatiwa angalau mche mmoja wa mti kwa ajili ya kupanda na kutunza”

Aidha CPA. Kashimba aliwaasa wastaafu hao watarajiwa kuzingatia yale waliyojifunza lakini kubwa kujiepusha na matapeli ili wastaafu hao watarajiwa waendelee kuishi maisha mazuri.

“Genge hili lina nguvu sana tusilipuuze, Mafao ndio turufu yetu ya mwisho tuyatunze.” Aliasa.

Akizungumzia uamuzi huo wa PSSSF, Msaatu mtarajiwa Bw. Laurian Mganga, alimpongeza Mkurugenzi Mkuu wa PSSSF CPA. Hosea Kashimba na uongozi mzima wa Mfuko huo kwa uamuzi wa kuwapatia elimu ya kujiandaa kabla ya kustaafu, lakini pia kuwapatia kila mstaafu mche mmoja wa kupanda ili kutunza mazingira.

Mkurugenzi Mkuu wa PSSSF, CPA. Hosea Kashimba, akiwa amebeba mche wakati wa zoezi la ugawaji miche kwa wastaafu watarajiwa pamoja na watumishi wa Mfuko huo.
Watumishi wa PSSSF wakiwa wamebeba miche ya miti tayari kwa zoezi la kuigawa kwa washiriki
Mtumishi wa PSSSF, Bi. Nelu Mwalugaja (kushoto), akigawa miche kwa wastaafu watarajiwa
Baadhi ya wastaafu wakiangalia miche waliyopewa
CPA. Kashimba, akizungumza na wastaafu watarajiwa wakati wa kufunga semina hiyo Septemba 12, 2023

CPA. Kashimba, akiagana na mmoja wa wastaafu watarajiwa mwishoni mwa semina hiyo.

CPA. Kashimba akiongozana na Mkurugenzi wa Uendeshaji PSSSF, Bw. Mbaruku Magawa baada ya kufunga semina hiyo.

Mkurugenzi wa Uendeshaji PSSSF, Bw. Mbaruku Magawa, akizungumza na wastaafu watarajiwa wa mkoa wa Dar es Salaam, Septemba 12, 2023.
Meneja Uhusiano na Elimu kwa Wanachama, PSSSF, Bw. James Mlowe, akizungumza na wastaafu watarajiwa wa mkoa wa Dar es Salaam, Septemba 12, 2023.
Mkurugenzi wa Fedha PSSSF, Bi. Beatrice Musa-Lupi (kushoto), akiteta jambo na Meneja Uhusiano na Elimu kwa Wanachama, Bw. James Mlowe.
Mkurugenzi wa Uendeshaji PSSSF, Bw. Mbaruku Magawa, akizungumza na washtaafu watarajiwa wa mkoa wa Dar es Salaam, Septemba 12, 2023.




Meneja wa PSSSF, Kanda ya Ilala, Bi. Uphoo Swai