May 5, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Prof Mkenda aonya watoto kufukuzwa shule

Na Joyce Kasiki,Timesmajira online,Dodoma

WAZIRI  wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof.Adolf Mkenda amesema pamoja na jitihada zinazofanyika za kuhakikisha watoto wanapata chakula shuleni ,lakini mtoto yeye asifukuzwe shuleni kwa kushindwa kuchangia chakula hicho.

Prof.Mkenda ametoa kauli hiyo wakati akifunga Mkutano wa Mwaka wa Pamoja wa Tathmini ya Sekta ya Elimu  uliofanyika jijini Dodoma.

“Maana ya Elimu bila ada  ni kwamba mtoto aende shuleni akasome bila kikwazo cha michango ya aina yoyote itakayomfanya mwanafunzi ashindwe kwenda shule kupata elimu.”alisema kwa mwanafunzi ushindwa lakini michango ya aina yoyote ile isiwe kikwazo kwa mwanafunzi kushindwa kupata elimu anayoistahili.”amesema Prof.Mkenda

Hata hivyo amewaasa wajumbe wa mkutano huo na viongozi mbalimbali,waendelee kuhamasisha wazazi watoe michango ya chakula na michango mingine, ila mtoto asirudishwe nyumbani kwa sababu tu hajachangia chakula.

Amesema  hakuna mtu yeyote anakataza kijiji,mtaa,Serikali, halmashauri kuchukua hatua dhidi ya mzazi ambaye hachangii chakula shuleni,lakini hakuna adhabu inayoruhusiwa ya kumtoa mwanafunzi shuleni kwa sababu mzazi kakataa kufanya kile ambacho jamii imekifanya.

Aidha,Prof.Mkenda amewaomba na kuwataka wadau wa Maendeleo sekta ya Elimu kuhakikisha wanatoa misaada inayoendana na jinsi sera ya Elimu inavyokwenda.

“Hatutaki kutapanya tapanya juhudi,tunataka tuzielekeze kule ambapo tunakwenda, Project yoyote tutakayo kubaliana na Shirika lolote lile tungependa kuliangalia linaendana vipi katika safari hii ya mageuzi ya Elimu” amesema Prof.Mkenda.